Ijumaa, 6 Mei 2016

LUGHA INAVYOWEZA KUTUMIKA KIROHO




LUGHA
Lugha ni kitu ambacho kinaweza kuwatambulisha watu na aina ya watu kulingana na kundi wanaloliwakilisha. Kwa maana hiyo unaweza kumtambua mtu na kundi lake kutokana na lugha anayoitumia.

Kuna lugha wanayoitumia watu wa dunia ambayo inawafanya wafanikiwe katika mambo ya dunia. Hali kadhalika tukiokoka tunapata lugha nyingine yaani ipo lugha ambayo ni tofauti na ya dunia ambayo inatufanya tufanikiwe katika mambo ya kiroho.

Ukiingia na lugha za dunia ndani ya wokovu huwezi kupata mpenyo katika mambo ya kiroho. Hii ni kwa sababu ndiyo inatambulisha watu na mfumo wao wa maisha.

Lugha inakuwezesha kutambua aina ya mtu unayeongea naye, lugha au maneno ya mtu hutengeneza taswira fulani ya maisha ambayo huumbika na hatimaye huja kutokea kweli.

Watu wengi hapa duniani wanaishi maisha ambayo waliyafikiria na kuyasema kabla hayajakuwa dhahiri. Unaposema sana juu ya jambo fulani, hatimaye jambo hilo huumbika na hatimaye hutokea hata kama hukulitaka.
Nguvu ya roho mtakatifu na roho chafu hutegemea sana mambo matatu ambayo ni;-
1.  Neno
2.  Imani
3.  Ukiri
Tukianza na neno, tunajifunza kwamba neno ni kama mwongozo wa jambo au ni kama katiba, ambayo ndani yake kuna maelekezo ya haki yako na wajibu wako kwa unayehusiana naye.

Kama vile ambavyo Mungu hutumia kitabu chake Biblia lakini pia hata shetani ana vitabu vyake anavyotumia ingawa pia shetani anaijua vizuri sana Biblia na haki za mtu aliyeokoka.
Katika matendo 19:18 – 20 tunaona habari kwamba kuna watu waliokuwa wanatumia vitabu kwa uganga wakavikusanya na kuvichoma.

IMANI.
Imani ni kuwa na uhakika wa jambo unalolitarajia, na katika mambo ya kiroho imani ni kitu cha lazima sana, hata wachawi hutumia imani ya kiwango cha juu sana katika kufanya kazi zao za kichawi. Hebu fikiria mwenyewe mtu anakaa kwenye ungo na anafanya mambo yake na hatimaye ungo unapaa na kuelekea anakotaka, jambo hili huwezi kulifanya kama una imani ya kubahatisha.

UKIRI.
Ukiri au usemi ni wa lazima sana katika mambo ya kiroho, unaweza kuwa una neno, na pia una imani ya kutosha, lakini bila kusema hakuna kinachoweza kufanyika. Maneno tunayokiri yana nguvu kubwa sana na ukiitumia vizuri ni lazima ushinde.

Wakati mfalme Daudi  anapambana na Goliathi, pamoja na Goliati kumuona Daudi kuwa ni kijana mdogo mwenye uso mzuri, lakini Goliati kuna maneno ambayo alimsemea kwamba angemuua na kuwapa ndege nyama yake.
Daudi naye wakati anamwendea Goliati naye alisema maneno ambayo yalikuwa mengi kuliko aliyoyasema Goliati, na aliahidi kukata kichwa chake na kwa upanga ijapokuwa hakuwa na upanga bali alikuwa na kombeo tu, lakini maneno yake yalitimia na akamkata kichwa Goliati kwa upanga wake mwenyewe.

Kila mara kabla ya ugomvi kutokea mara nyingi huanza na maneno, na mwenye maneno mengi mara nyingi hushinda , angalia hata kwa mabondia au wanamieleka.

Wakati wa vita vya kagera pia kulikuwa na maneno kabla ya vita kuanza. Idi Amin dada wa Rais wa Uganda wakati ule alisema atahakikisha chai anakunywa Mwanza, chakula cha mchana Dodoma na chakula cha usiku Dar es salaam. Amin hakufafanua atawezaje kufanya mambo hayo bila kutueleza ana uwezo kiasi gani.

Lakini kwa upande wa Tanzania Rais wa wakati huo mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akiongea na wazee wa Dar es salaam katika ukumbi wa Karimjee alisema maneno machache kwamba sasa tunampiga Amin, uwezo wa kumpiga tunao, nia ya kumpiga tunayo, na sababu za kumpiga tunazo.  Tunataka dunia ituelewe hivyo.

Na matokeo yake idi amini alipigwa na utawala wake kuangushwa.
Kwa sababu hiyo lugha zetu na za watu wa dunia ni lazima zitofautiane ili tuweze kufanikiwa katika mambo ya Mungu.
Ni lazima tujitofautishe na watu wa dunia wanavyokiri kuhusu uchumi, maisha, biashara, nk.

Hii ni kwa sababu lugha ndiyo inayotumika kusukuma nguvu ya Mungu, ni lazima tujue Biblia inatagiza kufanya nini kwa mfano tunapokuwa katika hali ya hasira, tukiwa na majirani, kazini, nyumbani kwenye familia n.k.
Biblia natuambia katika kitabu cha Mwanzo 11: 1 – 9 kwamba nchi yote ilikuwa na lugha moja na watu hawakutaka kutawanyika.

Waliamua kujenga mnara mrefu ufike mbinguni ili wasitawanyike. Walijenga mnara huu kwa kutumia lami na matofali, na Mungu alijua kwamba watafanikiwa kwa sababu ya hamasa waliyokuwa nayo. Kwa kawaida tulitegemea kwamba Mungu angewanyanganya lami na matofali, lakini hapana Mungu aliamua kuchukua lugha yao nah ii iliwafanya wasambaratike.

Nguvu ya watu hao haikuwa katika katika lami na matofali bali ilikuwa katika lugha na katika usemi, na Mungu alijua hakika kwamba wangefanikiwa. Kwa sababu ukiri wao ulikuwa katika usemi.

Angewanyanganya lami na matofali wangeweza kushauliana cha kufanya ili ujenzi wa mnara uendelee.
Lugha ndiyo inaymtambulisha mtu ni nani na ni wa kundi gani, kwa kutumia lugha unaweza kumjua kahaba, msomi, ameokoka n.k. kwa sababu lugha ndiyo inayomtambulisha mtu na kundi lake, lugha ndiyo inayomtambulisha mtu 

kama ni wa kufa au ni wa kuishi.
Katika kitabu cha Waamuzi 12: 5 – 6 kuna habari ya vita kati ya Wagileadi na Waefraimu na kuna askari aliyejichanganya na walimgundua kutokana na usemi, alishindwa kutamka neno shibolethi akasema siboleth.
Wakati wa matatizo ya Ayubu katika kitabu cha (Ayubu 2:9-10) Ayubu alimwambia mke wake ameongea kama  wanawake wapumbavu, kumbe wanawake wapumbavu nao wana lugha zao.

Katika injili ya Mathayo 26 tunasoma habari za Petro kwamba lugha yake ilimtambulisha kwamba yuko na Yesu.
Ukitaka kumshinda shetani ni lazima kwanza ubadilishe lugha unayotumia wakati unapoongea naye, huwezi kumshinda shetani kwa kutumia lugha yake.

Mithali 6: unakamatwa na maneno yako mwenyewe, katika kitabu cha Waamuzi 15:7 Samsoni alijiapiza kwa sauti kwamba atawapiga Wafilisti halafu atakoma.
Ni vizuri kwa waliookoka wakajifunza kwamba wasikubali kuwaacha watu wanawaongelesha mambo ya ajabu na wakakaa kimya
Mzee anapomwambia mtoto mchumba anamfunika katika ulimwengu wa roho .
MUNGU AKUBARIKI KWA KUFUATILIA SOMO HILI.
Furaha Amon   - Tanga  Mob: 0713 461593


Jumatano, 4 Mei 2016

VITA VYA KIROHO : SEHEMU YA KWANZA



 

Biblia inasema.

10 Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake.

11 Vaeni silaha zote za Mungu,mpate kuweza kuzipinga hila za shetani

12 kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka,juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.

13 kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu,mpate kuweza kushindana siku ya uovu,na mkiisha kuyatimia yote kusimama.

14 Basi simameni hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa darii ya haki kifuani,

15 nakufungiwa miguu utayari wa injili ya amani.

16 Zaidi ya yote mkitwaa ngao ya imani ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya Yule mwovu

17 tena ipokeeni chepeo ya wokovu, na upanga wa roho ambao ni neno la Mungu

18 kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika roho.  

Ili tuwe kulewa vizuri na kwa urahisi somo hili ni muhimu kuanza na mistari hii ya Biblia ili kujenga msingi wa somo hili.

Tunasoma hapa mtume Paulo anawaelezea Waefeso aina ya vita tunayopigana na namna ambavyo tunatakiwa kupigana kwa mbinu, maana vita si lelemama kwa hiyo ili tuweze kushinda tunahitaji kujifunza mbinu za kivita. Maisha ya wokovu sio maisha mepesi kama tunavyoaminishwa na baadhi ya wainjilisti kwamba kwa Yesu ni tambarare, hiyo sio kweli ukishaambiwa kuna vita na unatakiwa kupigana basi ni lazima ujue kwamba wewe sio raia bali ni askari. Na kwa kawaida askari ni raia aliyepewa mafunzo maalumu ya kupigana vita kwa kutumia zana mbalimbali za kivita. Ndio maana inakuwa muhimu sana kujifunza aina ya vita na mbinu ambazo zitatusaidia kupata ushindi. katika mstari wa 12 Mtume Paulo anasema  

12 kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.

Katika mstari huu Biblia inatujulisha kuhusu aina ya vita tunayopigana, tunapigana na nani, lakini pia ametufahamisha kuhusu aina mbili za ulimwengu, kwamba kumbe kuna ulimwengu wa damu na nyama ambao ndio dunia hii ambayo sisi tunayoishi.

Lakini pia kuna ulimwengu wa roho ambao sisi kwa macho na kwa akili za kawaida hatuwezi kuuona wala viumbe vinavyokaa katika ulimwengu huo hatuwezi kuviona katika macho ya kawaida, ulimwengu huo ndio ambao nataka tuuangalie kwa undani.

Inawezekana tukawa tunajua mambo machache kuhusu ulimwengu wa roho, lakini kwa uchache ulimwengu wa roho ndio ulimwengu halisi na dunia ni kivuli cha ulimwengu wa roho, ulimwengu huo ulikuwepo kabla ya dunia kuwepo na Mungu wakati anaiumba hii dunia alikuwa anaiumba akiwa katika ulimwengu wa roho.

Kwa kifupi ni kwamba ulimwengu wa roho ndio wenye nguvu kubwa sana kiasi cha kwamba dunia yetu pamoja na uzito wake wa mabilioni ya tani imeshikwa na nguvu kidogo sana kutoka katika ulimwengu wa roho, na inajizungusha yenyewe kwa masaa ishirini na nne kupata usiku na mchana. Lakini pia inalizunguka jua kwa siku 365 au 366 ili kupata mwaka bila kupoteza majira na mwelekeo wake. Watu wanaosoma elimu ya unajimu wanajua kwamba nguvu iliyoko katika ulimwengu wa roho inatawala maisha ya wanadamu walioko katika dunia hii tunayoishi.

Tangu zamani, wanadamu wamechunguza miendo hususa ya nyota na sayari katika mbingu za usiku na pia mahali tofauti-tofauti ambapo nyota na sayari hizo zinakuwa kulingana na majira.

Mungu akasema, na iwe mianga katika anga la mbingu ili itenge kati ya mchana na usiku; nayo iwe ndio dalili na majira na siku na miaka;        (Mwanzo 1:14)

Hata hivyo, iwe tunajua au hatujui, mienendo ya nyota na sayari ina uvutano wa moja kwa moja katika maisha yetu. Dunia huzunguka jua ambalo ni nyota inayotusaidia kujua urefu wa siku na mwaka. Mwezi ni “kwa ajili ya nyakati zilizowekwa,” au ‘kutupimia majira.

Aliufanya mwezi kwa ajili ya nyakati, jua latambua kuchwa kwake (Zaburi 104:19;

Nazo nyota ni mwongozo unaotegemeka katika usafiri, na hata wanaanga wanaweza kutumia nyota wanapoongoza vyombo vyao vya angani. Kwa hiyo, wengi wangependa kujua kama nyota zinaweza kufanya mengi zaidi ya kutuonyesha wakati na majira, na kutusaidia tuthamini kazi za uumbaji za Mungu. 

Je, nyota zinaweza kutusaidia kujua wakati ujao au kutuonya kuhusu majanga na misiba? Najaribu kukuchambulia nguvu ambayo iko katika ulimwengu wa roho.

Unajimu, ambao ni mazoea ya kutazama mbingu ili kutafuta ishara za kuongoza maisha yetu duniani, ulianzia Mesopotamia ya kale, yaelekea katika miaka ya 2000 K.W.K. Wanajimu wa kale walitazama mbingu kwa makini.

Elimu ya nyota ilianzishwa na juhudi zao za kuchora miendo ya nyota na sayari, kujua mahali kila nyota ilipo, kutengeneza kalenda na kutabiri kupatwa kwa jua au mwezi. Lakini wanajimu hawachunguzi tu uvutano wa mwezi na jua katika mazingira yetu. Wanajimu wanadai kwamba mpangilio wa jua, mwezi, sayari, nyota, na makundi ya nyota, una uvutano juu ya matukio makuu duniani na pia juu ya maisha ya kila mtu.

Wanajimu fulani wanatazama nyota na sayari ili wajue mambo au hatari za wakati ujao. Na watu wanaouelewa wanaweza kuutumia ujuzi huo na kunufaika nao kwa njia mbalimbali. Wengine wanahisi kuwa unajimu unaonyesha kile ambacho kimeamuliwa mapema tufanye. 

Sasa kwa sababu hiyo mtume Paulo anatuonya kwamba tusijaribu kushindana katika mwili maana kwa kufanya hivyo tunakuwa tumechelewa, kwa sababu mambo yote yanakuwa tayari yameshaamriwa katika ulimwengu wa roho na ni mpaka ujue namna ya kuingia katika ulimwengu wa roho na kupata habari hapo ndio unaweza kushindana. 

ninayo mambo mengi sana ya kushuhudia jinsi mambo ambayo niliyaona mapema katika ulimwengu wa roho yalikuja kutimia baada ya majuma au miezi kadhaa.

Watu wasiomjua Mungu unajimu unaweza kuwasaidia kujua wakati unaofaa wa kushiriki katika utendaji fulani au kuanza kufanya mambo fulani. 

Inasemekana kwamba habari hizi zinaweza kujulikana kwa kutazama mpangilio wa nyota au sayari fulani na kuchunguza uhusiano kati ya nyota na sayari hizo na pia uhusiano wake na dunia. 

Inasemekana kuwa uvutano wa nyota na sayari juu ya maisha ya mtu binafsi unategemea mpangilio wake wakati wa kuzaliwa kwa mtu huyo.

Wanajimu wa kale walifikiri kuwa dunia ndiyo kitovu cha ulimwengu, na kwamba sayari na nyota zilikuwa zimefungiwa katika miviringo ya kimbingu ambayo iliizunguka dunia. 

Pia walifikiri kwamba jua linasafiri angani kati ya makundi ya nyota likifuata njia fulani hususa katika mzunguko wa kila mwaka.

Waliigawanya njia hii ya jua ya kila mwaka katika sehemu au maeneo 12. Sehemu hizo zote zilikuwa na makundi ya nyota, na kila sehemu ilipewa jina kulingana na kundi la nyota ambamo jua lilipitia.

Sehemu hizo zikawa zile ishara 12 za nyota na kuitwa “nyumba za mbinguni,” kwa sababu zilionwa kuwa makao ya miungu. Hata hivyo, wanasayansi waligundua baadaye kuwa jua haliizunguki dunia bali dunia ndiyo inayozunguka jua. Uvumbuzi huo ulithibitisha kuwa unajimu si sayansi yenye kutegemeka.

Kutoka Mesopotamia ulikoanzia, unajimu ulienea hadi karibu sehemu zote za dunia na ukatumiwa kwa njia moja au nyingine katika maeneo yote yenye ustaarabu mkubwa duniani. Baada ya Uajemi kushinda Babiloni, unajimu ulienea hadi Misri, Ugiriki, na India. 

Kutoka India, wamishonari Wabudha waliueneza hadi Asia ya Kati, China, Tibet, Japani, na Asia ya Kusini-Mashariki. Yaonekana kuwa unajimu uliopo leo ulianzishwa huko Misri wakati wa utawala wa Ugiriki, na umeathiri sana maoni ya Wayahudi, Waislamu, na watu wa dini zinazojidai kuwa za Kikristo. 

Bado hata sasa  katika nchi nyingi watu hawatoki majumbani kwao bila kujua nyota yake inasemaje kuhusu siku hiyo, kwa hiyo ni lazima wapate magazeti yenye kurasa maalumu za watabiri wa nyota.

Wakati wa utawala wa Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, makuhani na wanajimu walishindwa kufasiri ndoto ya mfalme. Danieli, nabii wa Mungu wa kweli, alionyesha sababu zilizofanya washindwe kufasiri ndoto hiyo aliposema:

“Siri ambayo mfalme anauliza, watu wenye hekima, wala wafanya-mazingaombwe, wala makuhani wenye kufanya uchawi wala wanajimu hawawezi kumwonyesha mfalme. Hata hivyo, kuna Mungu mbinguni ambaye Ni Mfunuaji WA siri, naye amemjulisha Mfalme Nebukadneza mambo yatakayotokea katika siku za mwisho.” 

(Danieli 2:27, 28)

Danieli alimtumaini Mungu ambaye ni “Mfunuaji wa siri”— bali si jua, mwezi, au nyota—na akamweleza mfalme maana ya kweli ya ndoto yake.—Danieli 2:36-45

Kwa maana nyingine ni kwamba Mamlaka ya Mungu katika ulimwengu wa roho ilikwisha amua juu ya hatma ya ufalme wa Nebukadneza, kwa hiyo Nebukadneza hata angejitahidi kupambana wakati anguko lake linatokea angekuwa anapigana katika damu na nyama. 

ndipo mtume Paulo anakataa kwamba hatutakiwi kupigana katika damu na nyama. Ni sawa na kwamba tumesha chelewa.

Neno la Mungu linafunua wazi kwamba ‘matendo yenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu,’ ni “utendaji wa Shetani.”—2 Wathesalonike 2:9.

Kama vile ambavyo kuvuta bangi kunaweza kumfanya mtu awe mtumwa wa walanguzi wa dawa za kulevya, kujihusisha na unajimu kunaweza kumfanya mtu atawaliwe na yule mdanganyifu mkuu, Shetani. 

Hivyo basi, wale wanaompenda Mungu na kweli, wanapaswa kuukataa kabisa unajimu na badala yake kutii shauri hili la Biblia: “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema.”—Amosi 5:15.

Unajimu umeenea sana kwa sababu watu wanatamani kujua mambo ya wakati ujao. Je, inawezekana kujua mambo hayo? Ikiwa ndivyo, tunaweza kuyajua jinsi gani? Biblia inasema kwamba hatuwezi kujua ni nini ambacho kitampata kila mmoja wetu kesho, mwezi ujao, au mwaka ujao. (Yakobo 4:14)

Hata hivyo, Biblia inatufunulia mambo ambayo yatawapata wanadamu kwa ujumla wakati ujao. Inatuambia kwamba karibuni, Ufalme utakuja, kama tunavyoomba katika Sala ya Bwana.

Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu nao utasimama milele na milele 

(Danieli 2:44);  

Basi ninyi salini hivi: Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe,ufalme wako uje,mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni. 

Mathayo 6:9, 10)

 Pia inatuambia kwamba kuteseka kwa binadamu kutaisha hivi karibuni na hatutasumbuka tena.

 Maana tazama, mimi naumba mbingu mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. (Isaya 65:17;

tutaendelea 0713 461593