Jumamosi, 11 Februari 2017

JE NI SAWA KUSIKILIZA YANAYOSEMWA NA MAPEPO? (1)


Utangulizi;-

Somo langu leo linaanza kama swali, lakini nafikiri nitalimalizia kama ushauri usio na masharti ya kukulazimisha ukubali ushauri wangu. Siku moja nimekwenda mahali fulani kwenye kanisa fulani, nikakuta mtumishi mmoja yuko na mtu ambaye amepagawa na pepo wachafu. Lakini  kilichoniogopesha ni vile kuona yule mtumishi ameshika daftari na kalamu! Halafu anamuuliza yule pepo ambaye amempagaa yule mtu! wewe ni nani? Pepo anajibu mimi maimuna! Umetumwa na nani? Nimetumwa na mama yake mdogo. Mko wangapi? n.k. baada ya majibizano hayo na yule mgonjwa kurudi kwenye fahamu zake anaanza kumsomea yale majibizano, kama alivyoelekezwa na pepo, kwamba katumwa na nani na wako wangapi n.k. Sasa mambo kama haya mimi nikiita ni ya kipumbavu na yanafanywa na mawakala wa shetani ndani ya kanisa, watu wengine wanasema nakosea. Maana mimi sioni tofauti kati ya mpiga ramli na hawa watu. Kwa nini nione haya kumfananisha mtumishi wa aina hii na mganga wa kienyeji. Na hali ndio kwa sasa imeshamiri katika makanisa ambayo tunayaita ya kiroho, kwa kweli ni janga kwa kanisa

UMUHIMU WA KUFUATA USHAURI WA MUNGU.
Mara nyingi ninapopata nafasi maalumu ya kuhubiri au kufundisha masomo ya Biblia au semina. Huwa  namuomba Mungu kwa unyenyekevu mkubwa sana juu ya hitaji la wale watu ambao ninakwenda kuwahudumia, katika ufahamu wangu ninakuwa na maelfu ya masomo ambayo ninatamani kuyafundisha. Lakini mara nyingi huwa ninamuomba Mungu anisaidie kunipa kile anachotaka yeye watu wajifunze. Ninakumbuka siku moja nilikuwa nnaongea na rafiki yangu mmoja ambaye ni Askofu kuhusu umuhimu wa tabia hii, akaniunga mkono na akanishuhudia yeye mwenyewe jinsi Mungu alivyomuepusha na mtego mbaya sana ambao shetani alikuwa ameutega katika huduma yake. 

Anasema Mungu alimwelekeza kwenye semina fulani kwamba siku ya kwanza akipanda madhabahuni asifundishe kitu chochote bali aongoze maombi tu. Alijaribu kushindana na maelekezo hayo lakini hatimaye aliamua kutii sauti ya Mungu, na ndivyo alivyofanya.
Elizabet Yohana na Rejoice George
Na baadae mwisho wa hiyo semina ndio akagundua ni kwa nini Mungu alimshauri afanye hivyo. Anasema hilo kanisa wakati huo alikuwa ameitwa kwa mara ya pili, kwa sababu alipokwenda kwa mara ya kwanza alifanya semina ambayo ilifanikiwa sana. Mungu alifanya mambo makubwa sana. Karibu wiki yote ile makanisa mengine ilibidi yafungwe kwa muda kwa sababu washirika wao walikimbilia kwenda kupata huduma katika semina hiyo ambayo Mungu alishuka kwa nguvu sana. Mpaka semina hiyo inaisha watu walitamani siku zigande, Kwa hiyo Mchungaji wa kanisa hilo akawa amejipanga kwa ajili ya semina nyingine ambayo alitaka iwe kubwa zaidi kuliko ile iliyopita. Kwa hiyo maandalizi yakafanyika na hatimaye tarehe ikapangwa na mhubiri akataarifiwa. Siku  chache baada ya matangazo ya semina na mialiko kuanza kusambazwa kikatokea kituko!, Mwanakwaya mmoja wakiwa katika mazoezi ya kujiandaa na semina akaangushwa na mapepo! Na wale wenye ujuzi wa kukemea na kuuliza maswali wakaanza kazi. Lile pepo likajibu kwamba mimi niliwekwa humu na huyo mtumishi anayekuja kufundisha!.
Rev Martin Pyuza
Aliniweka alipokuja kufundisha kwa mara ya kwanza. Habari ile ikachukuliwa kama ilivyo na viongozi wa kwaya huku ikiwa imevuviwa na roho ya pepo, ikapelekwa kwa viongozi wengine wa kanisa, na hatimaye ikafika kwa Mchungaji kiongozi ikiwa na maelekezo ya kipepo na kupelekwa kama ombi la kufuta hiyo semina. Wakataka huyo askofu kabla hajafika atumiwe ujumbe haraka sana kwamba semina imeahirishwa. Mchungaji wao alikuwa vizuri zaidi kiroho, na mtu mwenye msimamo, akasema kama mtu angetoa unabii kupitia Roho Mtakatifu, bado Biblia inaturuhusu kuupima huo unabii. Akaona haiwezekani mapepo kumuelekeza jinsi ya  kufanya kazi ya Mungu.
nabii mmoja Afrika kusini akiwa katika maombezi
Pamoja na msukumo mkubwa uliokuwepo kutoka kwa wazee na viongozi wengine wa kanisa lile, Mchungaji yule akakataa kabisa kubadilisha kitu chochote akawaambia mimi pia nina Roho Mtakatifu, sio lazima shetani anielekeze. Wakati ulipofika yule Askofu akaja. Lakini akiwa katika maombi Mungu akamwambia siku ya kwanza usifundishe kitu chochote. Tumia kipindi kizima kufanya maombi. Yeye hakuelewa kitu chochote kinachoendelea mahali pale ila alikuwa mtii kwa Mungu wake. Baada ya kuimba nyimbo za kusifu na kuabudu, ndipo Mchungaji mwenyeji akapanda na hatimaye alimkaribisha Askofu kwa ajili ya kufundisha semina. Akaniambia alipopanda akaanzisha kawimbo ka kuabudu na kisha kuanza kunena kwa lugha, nguvu ya Mungu inashuka na kanisa zima linanena kwa lugha muda mrefu, akiona nguvu ya Mungu inapungua anaendeleza kale kawimbo kake nguvu ya Mungu inashuka tena kwa kasi kubwa, watu wananena kwa lugha mpaka wanaanguka wenye mapepo yanawatoka na wengine wanapokea uponyaji mubashara.
nabii mwingine akimlisha mtu nyoka kwenye maombi
Mpaka muda wake ulipoisha hakuna mtu aliyeweza kutoka nje. Kila mtu aliyefika siku ile akaamini kwamba yule aliyetenda yale ni Mungu. Siku iliyofuata ndio akaanza kufundisha masomo aliyopanga, watu walifunguliwa na kila mtu akaamini kwamba yule mwanakwaya, pengine bila kujua au kwa sababu ya kutokukaa vizuri na Mungu, alitumiwa na shetani kutaka kukwepa kipigo anachokipata. Mwisho wa semina ndio yule Mchungaji mwenyeji akamweleza kilichotokea. Na ndipo yeye akajua kwamba Mungu aliamua asifundishe ili alainishe kwanza mioyo ambayo ilitiwa sumu na shetani kupitia kwa yule mdada wa kwaya. Akaniambia angelazimisha kufundisha pengine watu wasingepokea kitu, kwa sababu walikuwa tayari wameshafunga mioyo yao, au shetani angeendelea kuwapa tafsiri tofauti ya fundisho lake, ili kuthibitisha maneno ya uwongo wa pepo wake.

KUNA WATUMISHI ITABIDI WAJE KANISANI NA TUNGULI
Iwapo kweli wewe mtumishi umeamua kukubali kutumia mapepo kwa ajili ya kuwatafutia watu wako uvumbuzi wa matatizo yao, huna tofauti na watu wanaoulizia mambo mbalimbali kutokana na mizimu.
tuko katika nyakati za hatari
Ukweli ni kwamba sasa hivi kanisa limeingiliwa sana na watu kama hao, na kwa sababu Yesu alisema kwamba tuyaache magugu yakue pamoja na ngano. Lakini si vibaya watu wa Mungu wakajua kabisa kwamba, pamoja na kwamba tumeambiwa tusiyang’oe kwa kila dalili hili ni gugu tujaribu kuliepuka. Nimeona mtu mmoja anajiita nabii. Mtu akifika kwake anaanza kumtabilia kama mganga wa kienyeji, Eti! Unakumbuka juzi ulikwenda kwa shangazi yako. Alikupa maji kwenye kikombe cha bati, uliporudi nyumbani ukasikia maumivu ya tumbo! Sasa Roho Mtakatifu huwa hafanyi vitu vya kipumbavu na kichonganishi kama hivyo.

Yeye ni Roho wa amani tena hfanyi hivyo kama hujatoa pesa anayokutajia bila kupungua. Sasa hiyo kama sio kuingiza biashara za mizimu kanisani ni nini?
Inawezekana tukawa hatuna maarifa sana ya kiroho, lakini mambo mengine hata akili ya kawaida inakataa kabisa kuamini kama ndipo kanisa lilipofikia. Siku moja mwanangu alitaka sana niongozane naye kwenda kwa nabii fulani maana amemweleza mambo mengi sana kuhusu mimi. Nilijaribu sana kumkwepa lakini siku moja nikaona busara ni kwenda naye ili nisimkatishe tamaa. Mimi najua hakika mafundisho yake hayawezi kunidhuru. Maana Biblia imenihakikishia kwamba nitakula kitu cha kufisha na hakitanidhuru. Kwa hiyo niliamua kwenda kujifunza maana huwa siamini hata kama mtu atauchambua ukoo wangu wote. Nilipofika nilianza kuona mambo ndivyo sivyo, kwanza mwanangu akaniambia kama una pesa kubwa tafuta chenji maana kila maombi yana sadaka. Na kweli ni kama wamejipanga kuhakikisha kwamba hakuna fedha inayobaki mfukoni kwa watu waliokuja. Pia nikaona kipande cha kitambaa cheupe, wenyewe wanasema kina upako wa mtumishi kwa hiyo ukikinunua unaweza kukitumia kwenye maombi mbalimbali. Mara kuna mafuta ya upako n.k.

Mambo haya ukiyaangalia kwa ujumla wake, unaona kabisa kwamba hawa jamaa wameshindwa kuwavalisha watu hirizi tu. Lakini mambo mengi ni kama waganga wa kienyeji tu. Mpaka hapo nafikiri ni juu yako wewe kuamua kama unaona busara kuwasikiliza  mapepo wakisema eti wametumwa na muhubiri fulani, halafu na wewe ukiamini ujue kwamba shetani anakuona kuwa wewe ni dhaifu sana. Shetani ni baba wa uongo, halafu wewe unategemea kuupata ukweli kutoka kwa shetani. Kama na wewe unafanya hivyo ujue hakika kuwa unamtumikia shetani, kanisa halijaanza leo kushambuliwa na watu wa aina hii. Kipindi fulani kuna kundi kubwa la vijana waliokuwa wanajifanya wametoka kuzimu au kwamba walikuwa wachawi wa kiwango cha juu, kwa hiyo wameokoka na sasa wanamtumikia Mungu. Katika kundi lile sikumbuki kama kuna aliyebaki kwenye wokovu mpaka leo! Lakini tuliwapokea na haraka sana tukawaamini tukawapa mpaka madhabahu watufundishe mambo yao ya kishirikina waliyokuwa wanayafanya kabla ya kuokoka na wengine mpaka wakaoa kanisani. Unakuta mtu anakwambia wakati mimi sijaokoka niliwahi kufanya hivi na vile. Au nilifanya mkataba huu na ule unamuuliza sasa baada ya hapo ulifanya nini ili kufuta ile mikataba uliyoichukua kuzimu. Utakuta hana jibu anabaki kujiumauma tu. Na hao ndio wapo makanisani leo wanajifanya kutabiri na kulielekeza kanisa la Mungu. Ukweli ni kwamba kanisa lipo kwenye giza nene ni lazima watu fulani wapaze sauti na kusema wazi kwamba hawa sio watumishi wa Mungu aliye hai

                         SOMO HILI LITAENDELEA

Ijumaa, 10 Februari 2017

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (13)


Mwanamume Anamfanyaje Mkewe Azini?
Ona maneno ya Yesu, kwamba,
“Yeyote amwachaye mkewe, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi.”
Hili tena linatufanya tuamini kwamba hakuwa anaweka sheria mpya ya kuoana tena, bali alikuwa anadhihirisha tu ukweli kuhusu dhambi ya mtu anayemwacha mkewe bila sababu nzuri. “Amfanya kuwa mzinzi.” Kuna wanaosema kwamba Yesu alikuwa anamzuia huyo mwanamke kuolewa tena, kwa sababu anasema huo ni uzinzi. Lakini si hivyo.
Mkazo uko kwenye dhambi ya mwanamume anayemwacha mkewe, kwamba, kwa sababu ya kile anachokitenda, mke wake atakuwa hana lingine la kufanya isipokuwa kuolewa tena, ambayo si dhambi kwa upande wake maana yeye ameathirika kutokana na ubinafsi wa mumewe.
Machoni pa Mungu ni kwamba, kwa kuwa mwanamume alimwacha mkewe na kumwingiza kwenye kuolewa tena, ni kama amemlazimisha aingie kitandani na mwanamume mwingine.

Basi, yule anayedhani hajatenda uzinzi anakuwa na hatia kwa uzinzi mara mbili – wa kwake na wa mkewe.
Yesu hakusema kwamba Mungu anamhesabu mke aliyeathiriwa na talaka kwamba ana hatia ya uzinzi, maana hiyo isingekuwa halali, tena ingekuwa haina maana kabisa kama huyo mke aliyeathiriwa asingeolewa.
Mungu angewezaje kusema kwamba ni mzinzi kama asingeolewa? Isingekuwa na maana kabisa. Basi, ni dhahiri kwamba Mungu anamhesabu huyo mwanamume kuwa na hatia kwa uzinzi wake mwenyewe na “uzinzi” wa mkewe, ambao kweli si uzinzi kwake maana ni ndoa ya pili ambayo ni halali kabisa.

Sasa – vipi kuhusu maneno ya Yesu yafuatayo kwamba, “na mtu akimwoa mwanamke aliyeachwa anazini”? Ni mawili tu yanayoweza kueleweka. Aidha Yesu alikuwa anaongeza hatia ya uzinzi wa tatu dhidi ya mtu anayedhani kwamba hajawahi kuzini (kwa sababu ile ile kama aliyotumia kuongeza hatia ya pili), au Yesu alikuwa anasema kuhusu huyo mwanamume anayemtia moyo mwanamke aachane na mumewe ili waoane, “asizini”. Kama Yesu alikuwa anasema kwamba mwanamume yeyote duniani anayemwoa mwanamke aliyeachwa anazini, basi kila mwanamume wa Israeli alizini katika kipindi cha miaka mia nyingi ambaye, katika kutimiza Torati ya Musa, alimwoa mwanamke aliyeachika. Ukweli ni kwamba kila mwanamume siku hiyo aliyekuwa anamsikiliza Yesu, aliyekuwa amemwoa mwanamke aliyeachika kwa kufuatana na Torati ya Musa, alikuwa na hatia ya kosa ambalo hakuwa na hatia yake muda mfupi kabla ya hapo, na Yesu akawa amebadilisha sheria ya Mungu hapo hapo. Tena, kila mtu katika wakati ujao ambaye alimwoa mtu aliyeachwa, kwa kuamini neno la Paulo katika barua yake kwa Wakorintho kwamba hilo si dhambi, alikuwa ametenda dhambi – ni mzinzi.

Jinsi Biblia ilivyo inapelekea mtu kumstahi sana mwanamume aliyeoa mwanamke aliyeachwa. Kama yeye ni mwathirika wa ubinafsi wa mume wake wa kwanza, asiye na hatia, ningemstahi sana mwanamume huyo, kama ambavyo ningemstahi sana mwanamume anayeoa mjane na kumtunza. Kama huyo mwanamke alikuwa na sababu ya kulaumiwa kwa talaka yake, bado ningemstahi sana kwa kuwa na moyo wa Kristo kwa kuamini kwamba kuna kilicho bora kwake, na kwa neema yake ya kukubali kusahau yaliyopita na kujaribu. Kwa nini mtu yeyote aliyesoma Biblia, mwenye Roho Mtakatifu ndani yake aamue kwamba Yesu alikuwa anamkataza kila mtu asioe au kuolewa na yeyote aliyeachika? Hilo linaingiaje kwenye ukweli kwamba Mungu ni mwenye haki – haki ambayo haimwadhibu yeyote kwa kuwa mwathirika – kama mwanamke ambaye anaachwa pasipo kuwa na kosa? Hoja kama hiyo inaingiaje kwenye ujumbe wa Injili, wenye kutoa msamaha na nafasi nyingine kwa wenye dhambi wanaotubu?

Biblia inasema tena na tena kwamba talaka inahusisha dhambi kwa mmoja au kwa wenzi wote wawili. Mungu hakukusudia mtu yeyote aachane na mwenzake katika ndoa, lakini kwa rehema Zake alitoa mwanya wa talaka kama uasherati ukitokea. Kwa rehema pia aliweka mpango kwa watu walioachika kuoa na kuolewa tena.
Kama si kwa sababu ya maneno ya Yesu kuhusu kuoa na kuolewa tena, hakuna msomaji yeyote wa Biblia ambaye angedhani kwamba kuoa na kuolewa tena ni dhambi (isipokuwa kwa habari za matukio mawili nadra sana katika agano la kale, na moja la nadra sana katika agano jipya, yaani, kuoa na kuolewa tena baada ya mtu kuachana na mwingine aliyeokoka). Ila, tumepata njia inayokubalika ya kulinganisha kile alichosema Yesu kuhusu kuoa na kuolewa tena, na sheria kali zaidi yenye kukataza kuoa au kuolewa tena kwa kila hali. Hii sheria haifanyi kazi kwa wale ambao wamekwisha achana na kuingia katika ndoa zingine (maana ni sawa na kurudisha mayai yaliyopikwa yawe mabichi), na ni moja ambaye ingesababisha mkanganyiko wa hali ya juu na kuwapelekea watu kuvunja sheria zingine za Mungu. Badal ayake, tumeona kwamba Yesu alikuwa anawasaidia watu kutambua unafiki wao. ALikuwa anawasaidia wale walioamini kwamba hawatazini kamwe waone kwamba walikuwa wanazini kwa njia zingine, kwa tamaa zao na kwa mtazamo wao mwepesi kuhusu sababu za kuachana.

Kama Biblia nzima inavyofundisha, msamaha hutolewa kwa wenye dhambi wanaotubu, bila ya kujali dhambi yao, na nafasi ya pili na ya tatu hutolewa kwa wenye dhambi – pamoja na walioachika. Hakuna dhambi katika kuoa na kuolewa tena kwa aina yoyote katika agano jipya, isipokuwa kwa mwamini aliyeachana na mwamini mwenzake. Na hilo halipaswi kutokea kwa sababu waamini wa kweli hawafanyi mambo ya uchafu, na kwa sababu hiyo hakuna sababu halali ya kuachana. Ikitokea kwa nadra, wote wawili wabaki kama walivyo au wapatane.

MWISHO WA SOMO LOTE

Mungu akuinue kwa kufuatilia somo hili.

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (12)


Tusisahau kwamba wale watu Yesu aliosema nao wakati akihubiri Mlimani pia walikuwa wameishi maisha yao chini ya ushawishi wa Mafarisayo wanafiki, waliokuwa viongozi na waalimu wa Israeli. Kama tulivyokwisha jifunza hapo mapema tulipotazama Mahubiri ya Mlimani, ni dhahiri kwamba sehemu kubwa ya yale ambayo Yesu alisema yalikuwa kama masahihisho tu ya mafundisho ya uongo ya Mafarisayo. Yesu hata aliwaambia watu kwamba hawataingia mbinguni ikiwa haki yao haitazidi ile ya waandishi na Mafarisayo (Mathayo 5:20), ambayo ilikuwa njia nyingine ya kusema kwamba waandishi na Mafarisayo walikuwa njiani kwenda jehanamu. Mwisho wa mahubiri yake, watu walishangazwa kwa sehemu kwa sababu Yesu alikuwa anafundisha kitofauti, “si kama waandishi wao” (Mathayo 7:29).
Mapema katika mahubiri Yake, Yesu aliweka wazi unafiki wa wale waliodai kwamba hawajawahi kuzini, ila wanatamani na kuachana na wenzi wao na kuoa tena. Akapanua maana ya uzinzi kwamba ni zaidi ya tendo la kimwili la dhambi baina ya watu wawili walio na ndoa. Na aliyosema yalikuwa wazi kabisa kwa yeyote mwenye akili nzuri na mkweli,
ambaye angefikiri kidogo tu. Lakini kumbuka kwamba, mpaka wakati wa mahubiri ya Yesu, wengi wa watu katika lile kundi wangekuwa na mawazo kwamba ilikuwa halali kwao kuachana “kwa sababu yoyote” ile. Yesu alitaka wafuasi Wake pamoja na wengine wote wajue kwamba kusudi la Mungu tangu mwanzo lilikuwa kiwango cha juu zaidi.
Mmesikia kwamba imenenwa, ‘Usizini’. Lakini mimi nawaambia, Kila mtu amtazamaye mwanamke kwa kumtamani amekwisha kuzini naye moyoni mwake. Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe. Kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanamu. Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe. Kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanmum. Imenenwa pia, ‘Mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka.’ Lakini mimi nawaambia, Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya usherati, amfanya kuwa mzinzi, na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini (Mathayo 5:27-32).
Kama tulivyokwisha ona mapema, ona kwamba maneno ya Yesu kuhusu talaka na kuoa tena yanafuata moja kwa moja maagizo aliyotoa kuhusu tamaa, hivyo kuyaunganisha pamoja. Tena, Yesu anasema vyote viwili ni uzinzi, na kuviunganisha zaidi. Basi tunaona kwamba kuna muunganiko wa kitu kinachofanana katika maelezo hayo ya fungu hili lote la Maandiko. Yesu alikuwa anawasaidia wafuasi Wake kuelewa maana ya kutii amri ya saba.
Maana yake ni kutotamani, na kutoachana na kuoana tena.
Kila mtu katika wasikilizaji Wake wa Kiyahudi alikuwa amesikia amri ya saba ikisomwa katika sinagogi (maana hawakuwa na Biblia binafsi siku zile), pamoja na mafafanuzi yaliyotolewa, na kuona jinsi waalimu wao – waandishi na Mafarisayo – walivyoyafanyia kazi maishani mwao. Ndipo Yesu akasema, “lakini mimi nawaambia”, ila hakuwa anataka kuongeza sheria zingine mpya. Yeye alitaka kudhihirisha tu mpango wa Mungu tokea mwanzo.
Kwanza – tamaa ilikuwa inakatazwa kabisa na amri ya kumi, na hata bila amri ya kumi, yeyote aliyefikiri vizuri angetambua kwamba ilikuwa ni kosa kutamani kufanya kitu ambacho Mungu amekataza.
Pili – tangu mwanzoni kabisa mwa kitabu cha Mwanzo, Mungu aliweka wazi kwamba ndoa ilitakiwa kuwa makubaliano ya maisha yote. Tena, yeyote aliyefikiri vizuri juu ya hilo angetambua kwamba kuachana na kuoana tena ni sawa tu na uzinzi, hasa kama mmoja atapanga kumwacha menzake kwa kusudi la kuoa tena.
Lakini tena katika mahubiri haya, ni wazi kwamba Yesu alikuwa anawasaidia tu watu waone ukweli kuhusu tamaa na ukweli kuhusu kuachana kwa sababu yoyote, na kuoana tena. Yeye hakuwa anaweka sheria mpya ya kuoana tena ambayo haikuwa “vitabuni” hadi wakati huo.
Inashangaza kwamba ni watu wachache sana kanisani ambao wamewahi kutimiza maneno ya Yesu ya kung’oa jicho au kukata mikono, maana mawazo hayo yanapingana sana na Maandiko mengine, na ni dhahiri kwamba kazi yake ni kutia nguvu hoja kuhusu kuepukana na kujaribiwa kuwa na mahusiano kimwili yasiyofaa. Lakini wengi sana kanisani wanajaribu kutafsiri moja kwa moja maneno ya Yesu juu ya yule mwenye kuoa au kuolewa tena kufanya uzinzi, hata ingawa tafsiri hizo zinapingana moja kwa moja na Maandiko mengine.
Lengo la yesu lilikuwa kuwafanya wasikilizaji Wake wakabiliane na ukweli, kwa tumaini kwamba talaka zingepungua baada ya hapo. Kama wafuasi Wake wangepokea moyoni yale aliyosema kuhusu tamaa, kusingekuwepo na uasherati au uchafu miongoni mwao. Kama usingekuwepo, kusingekuwepo na sababu halali za talaka. Basi, talaka isingekuwepo, kama Mungu alivyokusudia tangu mwanzo.
MWISHO WA SEHEMU HII

Tutakutana katika sehemu inayofuata ya somo hili Mungu akuinue kwa kufuatilia somo hili.

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (11)



Hebu tufikiri kuhusu watu wawili. Mmoja ana ndoa, ni mtu wa dini, anayedai kumpenda Mungu kwa moyo wake wote, ambaye ameanza kumtamani mwanamke kijana anayekaa jirani. Muda si muda anamwacha mkewe na haraka anamwoa yule msichana aliyemvutia.
Yule mwingine si mtu wa dini. Yeye hajawahi kusikia hata Injili, na anaishi maisha mabaya ambayo hatimaye yanaharibu ndoa yake.
Miaka kadhaa baadaye, akiwa peke yake tu, anaisikia Injili, anatubu, na anaanza kumfuata Yesu kwa moyo wake wote. Miaka mitatu baadaye anampenda mwanamke mwenye kumpenda Mungu sana anayekutana naye kanisani. Wote wawili wanatafuta mapenzi ya Mungu na ushauri wa wengine kwa bidii, kisha wanapanga kuoana. Wanakuja kuonana, na wanakuwa waaminifu kwa Bwana na wao kwa wao mpaka kifo.
Mr & Mrs Mziray
Sasa – hebu tudhanie kwamba wote wawili wametenda dhambi kwa kuoa tena. Katika hao wawili, ni yupi mwenye dhambi kubwa zaidi? Bila shaka ni yule wa kwanza. Yeye ni sawa na mzinzi tu.
Lakini – vipi kuhusu yule mtu wa pili? Je, ni kwamba ametenda dhambi? Je, tunaweza kusema kwamba yeye hana tofauti na mzinzi – kama yule wa kwanza? Hapana. Je, tumwambie yale ambayo Yesu alisema kuhusu watu wanaoachana na kuoa tena, na kumjulisha kwamba sasa anaishi na mwanamke ambaye Mungu hakumwunganisha naye kwa sababu anamhesabu bado ana ndoa na mke wake wa kwanza? Je, tumwambie kwamba anaishi katika zinaa?
Majibu yako dhahiri kabisa. Uzinzi hutendwa na watu ambao wameoana, wanaomwona mwingine asiyekuwa mwenzi wao. Kwa hiyo, kuachana na mwenzako kwa sababu umepata mrembo zaidi ni sawa na uzinzi. Lakini, mtu ambaye hajaoa hawezi kufanya uzinzi kwa sababu hana mwenzi wa kumkosea uaminifu, na mtu ambaye ameachika hawezi pia kutenda uzinzi kwa sababu hana mwenzi wa kumkosea uaminifu. Tukielewa mantiki ya kihistoria na kiBiblia kuhusu maneno ya Yesu, hatuwezi kufikia maamuzi yatakayopotosha watu, na yenye kupingana na Maandiko yote.

Wanafunzi waliposikia itikio la Yesu kwa jibu la Mafarisayo, walijibu hivi, “Kama mahusiano ya mwanamume na mke wake yako hivyo, ni afadhali kutokuoa” (Mathayo 19:10). Tambua kwamba walikuwa wamekulia chini ya mafundisho na ushawishi wa Mafarisayo, na katika utamaduni uliokuwa umeathiriwa sana na Mafarisayo. Hawakuwahi kudhani kwamba ndoa ni kitu cha kudumu kiasi hicho. Ukweli ni kwamba, muda mfupi uliopita, hata wao waliamini ni halali kwa mwanamume kumwacha mkewe kwa sababu yoyote. Basi kwa haraka wakaamua kwamba ingekuwa bora kuepukana na ndoa kabisa, ili kuepuka hatari ya kuachana na kuingia kwenye uzinzi. Yesu alijibu hivi:
Si wote wawezao kulipokea neno hili, ila wale waliojaliwa. Maana wako matowashi waliozaliwa hali hiyo toka matumboni mwa mama zao; tena wako matowashi waliofanywa na watu kuwa matowashi; tena wako matowashi waliojifanya kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni. Awezaye kulipokea neno hili, na alipokee (Mathayo 19:11-12).
Yaani – kinachoamua ni ile hamu ya kushirikiana kimwili aliyo nayo mtu, au uwezo wake wa kuitawala. Hata Paulo alisema hivi: “NI afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa” (1Wakor. 7:9). Wale waliozaliwa wakiwa matowashi au wale wanaofanywa matowashi na watu (kama ilivyokuwa zamani: watu waliwafanya wanaume wengine kuwa matowashi, ili wawape jukumu la kuwalinda wake zao) hawana hamu ya kushirikiana na mwanamke kimwili. Wale “wanaojifanya wenyewe kwa ajili ya ufalme wa mbinguni” ni wale ambao wamejaliwa na Mungu kipekee kuwa na uwezo wa kujitawala zaidi. Ndiyo maana “si wote wawezao kulipokea neno hili, ila wale waliojaliwa” (Mathayo 19:11).

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (10)


Huu ndiyo ufunguo wa kulinganisha maneno ya Yesu na ya Musa na ya Paulo. Yesu alikuwa anadhihirisha unafiki wa Mafarisayo tu. Hakuwa anaweka sheria inayozuia kuoa au kuolewa tena. Kama alikuwa anafanya hivyo, basi alipingana na Musa na Paulo, na kusababisha vurugu kwa mamilioni ya watu walioachika, na mamilioni ya watu walioingia kwenye ndoa nyingine. Kama Yesu alikuwa anaweka sheria kuhusu kuoa au kuolewa tena, tuwaambie nini wale ambao wameachika na kuoa au kuolewa tena kabla ya kusikia habari za Sheria ya Yesu? Je, tuwaambie kwamba wanaishi katika mahusiano ya kiasherati? Na, kwa kuwa tunajua Biblia inaonya kwamba hakuna wazinzi au waasherati watakaorithi ufalme wa Mungu (1Wakor. 6:9-10), tuwashauri kwamba waachane na wenzao? Pengine ni sawa, lakini, Mungu si anachukia kuachana?

Je, tuwaambie waachane kitandani mpaka wana ndoa wenzao wa kwanza wafe ili kuwaepusha na zinaa ya kila wakati? Lakini, Paulo si anawakataza wana ndoa kunyimana? Tena, ushauri kama huo si utapelekea watu kujaribiwa kimwili na hata kuamsha hamu za kutaka wana ndoa wenzao wafe?
Je, tuwaambie watu kama hao waachane na wenzao wa sasa na kurudiana na wenzao wa kwanza (kama wengine wanavyosema) – kitu ambacho kinakatazwa na Torati ya Musa katika Kumbukumbu 24:1-4?
Halafu – vipi kuhusu watu walioachana ambao hawajaoa tena? Kama wanaruhusiwa kuoa au kuolewa tena ikiwa wenzao walioachana nao walitenda uzinzi, nani atakayejizatiti kuthibitisha kama kweli uzinzi ulifanyika? Je, itabidi wana ndoa fulani wathibitishe kwamba wenzao walioachana nao walikuwa na hatia ya tamaa tu ili waweze kurudiana? Je, wengine itabidi watafute mashahidi wa kuthibitisha uasherati wa wenzao ili waweze kurudiana?
Kama swali lililopita – vipi kuhusu swala la mwenzi kuzini kwa sababu alikuwa katika ndoa na mtu aliyemnyima tendo la ndoa? Je, ni halali kwa huyo aliyekuwa anamnyima mwenzake tendo la ndoa aruhusiwe kuolewa, na yule mtu aliyezini akatazwe kuoa au kuolewa?
Vipi kuhusu mtu aliyezini kabla ya ndoa? Je, uzinzi wake huo si kukosa uaminifu kwa mwenzi wa baadaye? Je, dhambi hiyo hailingani na uzinzi, kama yeye au mwenzake wangekuwa katika ndoa wakati walipofanya dhambi yao? Mbona huyo aruhusiwe kuoa au kuolewa?

Vipi kuhusu watu wawili wanaokaa pamoja – bila ndoa – halafu wanatengana. Mbona wanaruhusiw akuoa na kuolewa na wengine baada ya kutengana, kwa kuwa hawakuwa na ndoa rasmi? Wana tofauti gani na wale wenye kuachana kisha wakaoa na kuolewa tena?
Vipi kuhusu kweli kwamba “mambo ya zamani yanapita” na “mambo yanakuwa mapya” wakati mtu anapo-okoka (ona 2Wakor. 5:17)? Je, inamaanisha kila dhambi iliyowahi kufanywa isipokuwa dhambi ya kuachana isivyo halali?
Yote hayo na maswali mengine mengi yanaweza kuulizwa, ambayo ni hoja zenye nguvu kabisa kuunga mkono wazo kwamba Yesu hakuwa anaweka sheria mpya kuhusu ndoa. Yesu alikuwa na akili za kutosha kutambua matokeo ya sheria Yake mpya ya ndoa kama ndivyo ilivyokuwa. Hilo tu linatosha kutuambia kwamba alikuwa anaweka wazi unafiki wa Mafarisayo – wanaume wenye tamaa, wanafiki, washika dini, waliokuwa wanaachana na wake zao “kwa sababu yoyote” na kuoa tena.
Sababu ya Yesu kusema kwamba walikuwa “wanazini” badala ya kusema tu kwamba walichokuwa wanafanya ni kosa ni kwa sababu alitaka wao waone kwamba talaka kwa sababu yoyote na kuoa tena baada ya hapo si tofauti na uzinzi, kitu ambacho wao walidai hawafanyi. Je, tuamue kwamba kitu pekee alichojali Yesu ni tendo la ndoa tu katika ndoa ya pili, na kwamba angeunga mkono ndoa ya pili mradi tu watu wasijihusishe katika tendo la ndoa? Hapana. Basi, tusimfanye aseme kitu ambacho hakumaanisha kusema.

MWISHO WA SEHEMU HII

Tutakutana katika sehemu inayofuata ya somo hili Mungu akuinue kwa kufuatilia somo hili.

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (9)



Usisahau Kwamba Yesu Alikuwa Anazungumza Na Mafarisayo. Baada ya kujua hayo, tutaelewa vizuri zaidi kilichokuwa kinamkabili Yesu. Mbele yake walisimama kundi la waalimu wa dini wanafiki, wengi ambao – kama si wote basi – walikuwa na talaka moja au zaidi, na pengine ni kwa sababu walikuwa wamepata wanawake warembo zaidi. (Si bahati kwamba maneno ya Yesu kuhusu talaka katika Mahubiri ya Mlimani yanafuata maonyo Yake makali sana kuhusu tamaa, na kusema ni aina ya uzinzi.) Na bado walikuwa wanajihesabia haki, wakidai kwamba wameishika Torati ya Musa.
Swali lao tu linadhihirisha jinsi walivyoegemea upande mmoja. Waliamini kabisa kwamba mtu angeweza kumwacha mke wake kwa sababu yoyote. Yesu akadhihirisha ufahamu wao mbovu wa kusudi la Mungu kuhusu ndoa kwa kurejea maneno ya Musa juu ya ndoa katika Mwanzo sura ya 2. Mungu hakukusudia kuwepo na talaka zozote, achilia mbali talaka “kwa sababu yoyote,” lakini viongozi wa Israeli walikuwa wanawaacha wake zao kiholela tu!
Inaonekana Mafarisayo walijua tayari msimamo wa Yesu kuhusu talaka, maana alikwisha kuutamka hadharani. Basi wakawa na pingamizi tayari:
“Mbona basi Musa aliagiza apewe hati ya talaka na kumwacha?” (Mathayo 19:7).
Hapo tena swali lao linaonyesha jinsi walivyogemea upande mmoja. Limeulizwa kana kwamba Musa alikuwa anawaagiza wanaume wawaache wake zao baada ya kugundua “neno ovu,” mradi tu watoe hati ya talaka. Lakini, kama tujuavyo kutokana na Kumbukumbu 24:1-4, Musa hakusema hivyo hata kidogo. Yeye alikuwa anaweka sawa ndoa ya tatu ya mwanamke – akimzuia asiolewe tena na mume wake wa kwanza.

Kwa vile Musa alitaja talaka, bila shaka talaka ilikuwa inaruhusiwa kwa sababu fulani. Lakini ona kwamba neno alilotumia Yesu katika jibu lake – aliruhusu – ni tofauti na chaguo la Mafarisayo – aliamuru. Musa aliruhusu talaka, hakuamuru. Na sababu ya Musa kuruhusu talaka ni ugumu wa mioyo ya Waisraeli. Yaani – Mungu aliruhusu talaka kama tendo la huruma tu kwa hali ya dhambi ya watu. Alijua watu wasingekuwa waaminifu kwa wana ndoa wenzao. Alijua uchafu ungekuwepo. Alijua mioyo ya watu ingevunjika. Basi, akatoa ruhusa kwa talaka. Hakuwa amekusudia hivyo tangu mwanzo, lakini dhambi ililazimisha hivyo.
Kisha Yesu akaweka sheria ya Mungu wazi kwa Mafarisayo, akifafanua kile ambacho Musa anakiita “neno ovu”.
“Yeyote amwachaye mkewe, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, akamwoa mwanamke mwingine, azini” (Mathayo 19:9).
Machoni pa Mungu, uzinzi ndiyo sababu halali pekee kwa mwanamume kumwacha mke wake. Na ni rahisi kueleweka. Ni kitu gani kingine ambacho mwanamume au mwanamke anaweza kufanya, kikawa kibaya kwa mwenzake kuliko hicho? Mtu anapozini, anatuma ujumbe mchungu sana. Kwa hakika Yesu hakuwa anazungumzia uzinzi tu aliposema hayo. Bila shaka hata kumbusu mwenzi wa mwingine na kumshika-shika ni kitu kibaya sana, kama ilivyo tabia ya kuangalia picha mbaya za ngono, au matendo mengine yasiyofaa ya mahusiano kimwili. Kumbuka kwamba Yesu alifananisha tamaa na uzinzi katika Mahubiri Yake ya Mlimani.
Tusije kusahau Yesu alikuwa anasema na nani – ni Mafarisayo waliokuwa wanaachana na wake zao kwa sababu yoyote na kuoa haraka haraka, lakini hao hao wasingezini kamwe ili wasivunje amri ya saba. Yesu aliwaambia wanajidanganya wenyewe. Walichokuwa wanafanya hakikuwa tofauti na uzinzi. Ndiyo ukweli huo. Yeyote aliye mkweli anaweza kuona kwamba mwanamume anayemwacha mkewe ili amwoe mwanamke mwingine anafanya kitu ambacho mzinzi hufanya. Tofauti ni kwamba, huyu mwingine anahalalisha uzinzi wake.

MWISHO WA SEHEMU HII YA SOMO

Tutakutana katika inayofuata ya somo hili Mungu akuinue kwa kufuatilia somo hili.

Jumanne, 7 Februari 2017

SOMO: UFUNUO WA NENO LA MUNGU (1)


Mwl F Amon


Utangulizi;
Neno la Mungu ni mwamba, na mtu aliyejengwa kwenye mwamba hata kama majaribu makubwa yatakuja atayashinda. Neno la Mungu ambalo ni mwamba ni Rhema sio logos. Neno la Mungu ambalo linao uwezo wa kumuimarisha na kumjenga mtu ni Rhema. Rhema ndilo neno ambalo humbadilisha mtu hii ndilo neno la ufunuo. Biblia inasema;-
“Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba. Mvua ikanyesha mafuriko yakaja, pepo zikavuma zikaipiga nyumba ile isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asifanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile ikaanguka, nalo anguko lake likawa kubwa” (Mathayo 7:24  27)
wakati mtu anasikiliza neno la Mungu likihubiriwa wakati huohuo ndani yako huwa kuna sauti ya Mungu inayolifafanua hilo neno linalohubiriwa. Ufafanuzi huu hulenga mahitaji ya muhusika. Hii hutokea hata wakati unapokuwa unasoma Neno la Mungu. Sauti hii ndio ambayo huwa inafafanua neno la Mungu ndani ya mtu. Hii ndiyo Rhema huo ndio ufunuo wa neno la Mungu
”kufafanusha maneno yake kuwatia nuru, na kumfahamisha mjinga” (Zaburi 119: .)
Wakati unasoma neno au unasikiliza mahubiri, ingawaje mhubiri atakuwa anahubiri katika somo fulani jingine, wakati huohuo Mungu anakuwa anazungumza na wewe juu ya jambo jengine tofauti moyoni mwako.
Mungu hutumia maneno yanayohubiriwa kuzungumza na wewe kwa kulipua ufunuo mwingine kupitia neno hilo linalohubiriwa. Lile linalofunuliwa kwako, hilo ndilo Mungu analolitaka kwako. Hilo ndilo neno linalobadilisha, ndilo linalokujenga na kukuimarisha. Hili ndilo unatakiwa ujengwe kwake. Hiyo ndio sauti ya Mungu kwako ikisema na wewe moja kwa moja, hilo ndilo neno unalotakiwa ulizingatie na kulishika. Hilo neno ni Roho, lina uwezo lina nguvu. Mtu anayelishika hilo neno na kulitenda huyu ndiye atakayesitawi na kuwa sawa na mbegu iliyopandwa katika udongo. Huyu ndiye ambaye amejengwa katika mwamba.

biblia haijui shida zako,wala muhubiri hazijui shida zako. Mungu pekee ndiye anayezijua. Anataka kukutana nazo,hivyo Mungu anazungumza na wewe wakati neno la Mungu linahubiriwa. Atazungumza na wewe kwa njia ya ufunuo,mkristo hujengeka kiroho kupitia ufunuo.ufunuo ni sauti ya Mungu ni neno la Mungu. Ufunuo ni Yesu Kristo mwenyewe.
wakristo wameshindwa kukua kiroho na shida zao zimeendelea kuwepo japokuwa wanahudhuria kanisani kila leo. Ni kwa sababu hawajasikiliza nini Mungu anachosema nao. Bali wamechukua kauli za viongozi wao wa dini kuwa ndilo neno la Mungu. Wamechukua mahubiri pekee wakauacha ufunuo unaolipuliwa ndani yao wakati neno linapohubiriwa. neno la mungu kwako ni ile tafsiri inayotolewa na roho mtakatifu ndani yako. Ni lile neno la Mungu unalolisikia ndani yako kupitia sauti ya Mungu wakati ukisikiliza neno linahubiriwa. Sina maana kuwa mahubiri si chochote si lolote, hapana! Mahubiri ni kibebeo cha neno la Mungu. Ndani ya mahubiri ndiko kuna neno lenyewe halisi la Mungu. mfano mpunga huwezi kuula ni mpaka ukobolewe kwanza ili utoke mchele ambao ndio hupikwa na kuliwa. Kwa maana hiyo huwezi kupika mpunga halafu ule. Hivyo hivyo kuna tofauti kati ya mahubiri na ufunuo. 
Mahubiri ni chakula ambacho hakijakobolewa, ufunuo ni chakula ambacho kipo tayari kwa kuliwa. wakristo wengi wamekuwa sio waangalifu. baada  ya unabii kutolewa na watumishi wa Mungu kuhusu eneo fulani la maisha yao, wao wameuchukua unabii huo moja kwa moja kama Mungu amesema nao. Wengi wao baadaye mambo yao hayakwenda kama unabii ulivyosema, wameathirika kiroho na kukatishwa tamaa kwa hilo.
Baada ya unabii uliotolewa kuusikia, je, wewe muhusika sauti ya Mungu ndani yako imesemaje? Hata kama baada ya kusikia kauli za viongozi wa dini au kupitia unabii uliotolewa, wewe nenda ukateketeleze uliyoyasikia kutoka kwa Mungu kupitia unabii huo au kupita kauli hizo za viongozi wadini. Pindi majaribu yakija Mungu mwenyewe atapigana na majaribu hayo, maana ni yeye ndiye aliyekuagiza kufanya.
Mungu ana kawaida ya kuyapigania aliyoyasema yeye mwenyewe. Hivyo ukiwekeza katika yale uliyoyasikia kutoka kwa Mungu utakuwa umejenga katika mwamba kwa jinsi hii ni lazima ufanikiwe.
Kuna wakristo wanaooana kwa kauli za viongozi wao wa dini, majaribu yanapokuja kwenye ndoa zao huwa wanashindwa kustahimili. Wengine wanafanya biashara kwa kauli za viongozi wao wa dini n.k. Majaribu yatakapokuja hawawezi kustahimili. Sikiliza ufunuo unaolipuliwa ndani yako kupitia hizo kauli, mahubiri na nabii, ufunuo huo ndio uufanyie kazi.
Majaribu huja ili yakutoe katika mpango wa Mungu. Kama unafanya au kama uko mahali ambapo si mpango wa Mungu, majaribu yakija yatakutoa na kukuweza. Kama unachofanya au kama pale ulipo uliagizwa na Mungu, majarbu yakija hayawezi kukutoa kwenye mpango huo. Maana huo mpango umejengwakwenye neno la Mungu ambalo ndilo mwamba.
Majaribu yanapokuja, dhoruba, misukosuko huwachanganya watu kiasi wanaanza kuona kuwa huenda Mungu hakuongea nao wafanye hilo jambo. Lakini iwapo Mungu alizungumza na wewe hata kama yakija majaribu mazito ni lazima utashinda, lakini iwapo hukusikia kutoka kwa Mungu ni lazima utashindwa na majaribu hayo, maana Mungu hatakuwa pamoja na wewe.
                                     
                     MUNGU WANGU AKUBARIKI SANA

                               Somo litaendelea. 

SOMO: MALAIKA—WATUMISHI WA MAISHA YETU (1)


Furaha Amon

Utangulizi;


Biblia hutaja habari za malaika zaidi ya mara mia tatu. Hata hivyo, watu wengi hawaamini uwepo wao. Isipokuwa katika  siku hizi za karibuni watu wameanza kukubali kwamba kuna viumbe vitakatifu vinavyoweza kuonekana kwa macho.
Ukweli unaonyesha kwamba mara nyingi mkazo wa mafundisho yetu unalenga zaidi kuwafundisha watu juu ya uwepo wa shetani na majeshi yake ya pepo wabaya. Ni muhimu kuwafundisha watu wajue kwamba kama kuna jeshi la pepo wabaya, wajue pia kuna jeshi la Malaika Watakatifu ni vizuri kujifunza na kujua namna ya kuwatumia.
Unapotaka kuandika habari kuhusu Malaika ni ngumu sana kupata msaada kutoka katika maktaba kwa sababu hakuna waandishi walioandika habari za kutosha kuhusu malaika na kwa kweli tunakuwa hatuitendei haki dunia na hasa kizazi kinachokuja. Hebu fikiria jinsi ambavyo barua chache za Mtume Paulo jinsi ambavyo zimesaidia ulimwengu kwa karne nyingi. Kwa hiyo kama tutajifunza na kuwafundisha wengine kuhusu habari za malaika tutakuwa tumeweka misingi muhimu sana kwa watu kuendelea kufuatilia na kushuhudia kuhusu namna ya kupata huduma za mawakili
Akifafanua maono aliyoona kuhusiana na malaika wa Mungu, nabii Danieli aliandika hivi: “Kulikuwa na maelfu elfu [ya malaika] walioendelea kumtumikia [Mungu], na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Danieli 7:10) Mstari huo unaonyesha kusudi la Mungu la kuwaumba malaika. Waliumbwa ili wamtumikie, nao wako tayari kutimiza maagizo yake.

Wakati mwingine Mungu huwatumia malaika kufanya mambo fulani yanayowahusu wanadamu. Katika somo hili nitazungumzia zaidi jinsi anavyowatumia kuwaimarisha na kuwalinda watu wake, kupeleka ujumbe kwa wanadamu, na kutekeleza hukumu yake juu ya waovu.
Nakumbuka siku moja nilipata safari, kwenda katika mji fulani mkubwa. ilikuwa ni safari ya kawaida ambapo niliagizwa kumwakilisha mkuu wangu wa dini, kufanya kazi fulani za kiroho ambazo ilikuwa azifanye yeye. kwa sababu gharama yote ya safari ilichukuliwa na kanisa, na mimi nikaona gharama hii isiende bure nikaona muda huohuo kufundisha semina japo siku tatu, yaani Ijumaa, Jumamosi na nimalizie siku ya jumapili mchana kisha nirudi zangu. kwa hiyo nilikuwa na muda wa kujiandaa kwa ajili ya huduma ambayo nitakwenda kuifanya huko. sikumbuki nilifundisha somo gani! ila nakumbuka usiku mmoja ndio Mungu alinipa neema ya kuwaona viumbe hawa watakatifu, walikuwa wamenizunguka na ninaimba nao wimbo wa kitabuni ambao unaitwa "Ni tabibu wa karibu" kwa kweli ni ngumu sana kuelezea katika maandishi msisimko nilioupata na kutamani kuendelea kuwa nao. Lakini kulikuwa na nuru ya ajabu inamulika kutoka mbinguni huku hao maraika wakishuka na kupanda. kwa kifupi nilimwona Bwana na semina ilikuwa sio ya kawaida. kwa mara ya kwanza ndio niliona kanisa zima wanagalagala chini kwa jinsi Mungu alivyotutembelea.

Malaika Huimarisha na Kulinda
Tangu viumbe hawa wa rohoni waliposhuhudia kuumbwa kwa dunia na Mungu kuwaumba wanadamu wa kwanza, Malaika wameonyesha ushirikiano na kwamba wanapendezwa sana na wanadamu. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu Kristo alisema hivi: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.” (Methali 8:31) Biblia inatuambia kwamba “malaika wanatamani
kuchungulia” mambo yanayomhusu Kristo na mambo ya wakati ujao ambayo yamefunuliwa kwa manabii wa Mungu.—1 Petro 1:11, 12.
Kadiri muda unavyopita, malaika wameona kwamba wanadamu wengi hawamtumikii Muumba wao mwenye upendo. Hilo limewahuzunisha sana malaika waaminifu! Kwa upande mwingine, mtenda-dhambi mmoja anapotubu na kugeuka kumwelekea Yehova, “shangwe hutokea kati ya malaika.” (Luka 15:10) Malaika wanawahangaikia sana wale wanaomtumikia Mungu, na Yehova amewatumia tena na tena kuwaimarisha na kuwalinda watumishi wake waaminifu hapa duniani. (Waebrania 1:14) Fikiria mifano kadhaa.

Malaika wawili walimsaidia Loti na binti zake kuokoka uharibifu kwa kuwatoa nje ya Sodoma na Gomora, yale majiji maovu.* (Mwanzo 19:1, 15-26) Karne nyingi baadaye, ingawa nabii Danieli alitupwa ndani ya shimo la simba, hakuumizwa. Kwa nini? Alisema hivi: “Mungu wangu mwenyewe alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:22) Malaika walimsaidia Yesu mwanzoni mwa huduma yake duniani. (Marko 1:13) Muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu, malaika alimtokea na “akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Msaada wa malaika ulimtia Yesu moyo sana hasa wakati huo muhimu maishani mwake! Pia, malaika alimfungua mtume Petro kutoka gerezani.—Matendo 12:6-11.

Je, malaika hutulinda leo? Tukimwabudu Yehova kulingana na Neno lake, tunaweza kuwa na
uhakika kwamba malaika wake wenye nguvu wasioonekana watatulinda. Biblia inaahidi hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.”—Zaburi 34:7.
Hata hivyo, ni lazima tukumbuke kwamba malaika wanamtumikia Mungu wala si wanadamu. (Zaburi 103:20, 21) Wanafuata mwongozo wa Mungu bali si maagizo au maombi ya wanadamu. Hivyo, Yehova Mungu ndiye tunayepaswa kuomba msaada, si malaika. (Mathayo 26:53) Bila shaka, kwa kuwa hatuwaoni malaika, hatuwezi kujua ni kwa kadiri gani Mungu huwatumia kuwasaidia watu katika hali mbalimbali. Lakini tunajua kwamba Yehova ‘huonyesha nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9; Zaburi 91:11) Tuna uhakika kwamba “hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye [Mungu] hutusikia.”—1 Yohana 5:14.

Pia, Maandiko yanatuambia kwamba sala zetu na ibada yetu inapaswa kuelekezwa kwa Mungu peke yake. (Kutoka 20:3-5; Zaburi 5:1, 2; Mathayo 6:9) Malaika waaminifu hututia moyo tufanye hivyo. Kwa mfano, wakati mtume Yohana alipotaka kumwabudu malaika fulani, kiumbe huyo wa roho alimkaripia na kumwambia hivi: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Mwabudu Mungu.”—Ufunuo 19:10.

                   SOMO HILI LITAENDELEA