Ijumaa, 10 Februari 2017

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (13)


Mwanamume Anamfanyaje Mkewe Azini?
Ona maneno ya Yesu, kwamba,
“Yeyote amwachaye mkewe, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi.”
Hili tena linatufanya tuamini kwamba hakuwa anaweka sheria mpya ya kuoana tena, bali alikuwa anadhihirisha tu ukweli kuhusu dhambi ya mtu anayemwacha mkewe bila sababu nzuri. “Amfanya kuwa mzinzi.” Kuna wanaosema kwamba Yesu alikuwa anamzuia huyo mwanamke kuolewa tena, kwa sababu anasema huo ni uzinzi. Lakini si hivyo.
Mkazo uko kwenye dhambi ya mwanamume anayemwacha mkewe, kwamba, kwa sababu ya kile anachokitenda, mke wake atakuwa hana lingine la kufanya isipokuwa kuolewa tena, ambayo si dhambi kwa upande wake maana yeye ameathirika kutokana na ubinafsi wa mumewe.
Machoni pa Mungu ni kwamba, kwa kuwa mwanamume alimwacha mkewe na kumwingiza kwenye kuolewa tena, ni kama amemlazimisha aingie kitandani na mwanamume mwingine.

Basi, yule anayedhani hajatenda uzinzi anakuwa na hatia kwa uzinzi mara mbili – wa kwake na wa mkewe.
Yesu hakusema kwamba Mungu anamhesabu mke aliyeathiriwa na talaka kwamba ana hatia ya uzinzi, maana hiyo isingekuwa halali, tena ingekuwa haina maana kabisa kama huyo mke aliyeathiriwa asingeolewa.
Mungu angewezaje kusema kwamba ni mzinzi kama asingeolewa? Isingekuwa na maana kabisa. Basi, ni dhahiri kwamba Mungu anamhesabu huyo mwanamume kuwa na hatia kwa uzinzi wake mwenyewe na “uzinzi” wa mkewe, ambao kweli si uzinzi kwake maana ni ndoa ya pili ambayo ni halali kabisa.

Sasa – vipi kuhusu maneno ya Yesu yafuatayo kwamba, “na mtu akimwoa mwanamke aliyeachwa anazini”? Ni mawili tu yanayoweza kueleweka. Aidha Yesu alikuwa anaongeza hatia ya uzinzi wa tatu dhidi ya mtu anayedhani kwamba hajawahi kuzini (kwa sababu ile ile kama aliyotumia kuongeza hatia ya pili), au Yesu alikuwa anasema kuhusu huyo mwanamume anayemtia moyo mwanamke aachane na mumewe ili waoane, “asizini”. Kama Yesu alikuwa anasema kwamba mwanamume yeyote duniani anayemwoa mwanamke aliyeachwa anazini, basi kila mwanamume wa Israeli alizini katika kipindi cha miaka mia nyingi ambaye, katika kutimiza Torati ya Musa, alimwoa mwanamke aliyeachika. Ukweli ni kwamba kila mwanamume siku hiyo aliyekuwa anamsikiliza Yesu, aliyekuwa amemwoa mwanamke aliyeachika kwa kufuatana na Torati ya Musa, alikuwa na hatia ya kosa ambalo hakuwa na hatia yake muda mfupi kabla ya hapo, na Yesu akawa amebadilisha sheria ya Mungu hapo hapo. Tena, kila mtu katika wakati ujao ambaye alimwoa mtu aliyeachwa, kwa kuamini neno la Paulo katika barua yake kwa Wakorintho kwamba hilo si dhambi, alikuwa ametenda dhambi – ni mzinzi.

Jinsi Biblia ilivyo inapelekea mtu kumstahi sana mwanamume aliyeoa mwanamke aliyeachwa. Kama yeye ni mwathirika wa ubinafsi wa mume wake wa kwanza, asiye na hatia, ningemstahi sana mwanamume huyo, kama ambavyo ningemstahi sana mwanamume anayeoa mjane na kumtunza. Kama huyo mwanamke alikuwa na sababu ya kulaumiwa kwa talaka yake, bado ningemstahi sana kwa kuwa na moyo wa Kristo kwa kuamini kwamba kuna kilicho bora kwake, na kwa neema yake ya kukubali kusahau yaliyopita na kujaribu. Kwa nini mtu yeyote aliyesoma Biblia, mwenye Roho Mtakatifu ndani yake aamue kwamba Yesu alikuwa anamkataza kila mtu asioe au kuolewa na yeyote aliyeachika? Hilo linaingiaje kwenye ukweli kwamba Mungu ni mwenye haki – haki ambayo haimwadhibu yeyote kwa kuwa mwathirika – kama mwanamke ambaye anaachwa pasipo kuwa na kosa? Hoja kama hiyo inaingiaje kwenye ujumbe wa Injili, wenye kutoa msamaha na nafasi nyingine kwa wenye dhambi wanaotubu?

Biblia inasema tena na tena kwamba talaka inahusisha dhambi kwa mmoja au kwa wenzi wote wawili. Mungu hakukusudia mtu yeyote aachane na mwenzake katika ndoa, lakini kwa rehema Zake alitoa mwanya wa talaka kama uasherati ukitokea. Kwa rehema pia aliweka mpango kwa watu walioachika kuoa na kuolewa tena.
Kama si kwa sababu ya maneno ya Yesu kuhusu kuoa na kuolewa tena, hakuna msomaji yeyote wa Biblia ambaye angedhani kwamba kuoa na kuolewa tena ni dhambi (isipokuwa kwa habari za matukio mawili nadra sana katika agano la kale, na moja la nadra sana katika agano jipya, yaani, kuoa na kuolewa tena baada ya mtu kuachana na mwingine aliyeokoka). Ila, tumepata njia inayokubalika ya kulinganisha kile alichosema Yesu kuhusu kuoa na kuolewa tena, na sheria kali zaidi yenye kukataza kuoa au kuolewa tena kwa kila hali. Hii sheria haifanyi kazi kwa wale ambao wamekwisha achana na kuingia katika ndoa zingine (maana ni sawa na kurudisha mayai yaliyopikwa yawe mabichi), na ni moja ambaye ingesababisha mkanganyiko wa hali ya juu na kuwapelekea watu kuvunja sheria zingine za Mungu. Badal ayake, tumeona kwamba Yesu alikuwa anawasaidia watu kutambua unafiki wao. ALikuwa anawasaidia wale walioamini kwamba hawatazini kamwe waone kwamba walikuwa wanazini kwa njia zingine, kwa tamaa zao na kwa mtazamo wao mwepesi kuhusu sababu za kuachana.

Kama Biblia nzima inavyofundisha, msamaha hutolewa kwa wenye dhambi wanaotubu, bila ya kujali dhambi yao, na nafasi ya pili na ya tatu hutolewa kwa wenye dhambi – pamoja na walioachika. Hakuna dhambi katika kuoa na kuolewa tena kwa aina yoyote katika agano jipya, isipokuwa kwa mwamini aliyeachana na mwamini mwenzake. Na hilo halipaswi kutokea kwa sababu waamini wa kweli hawafanyi mambo ya uchafu, na kwa sababu hiyo hakuna sababu halali ya kuachana. Ikitokea kwa nadra, wote wawili wabaki kama walivyo au wapatane.

MWISHO WA SOMO LOTE

Mungu akuinue kwa kufuatilia somo hili.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni