Jumanne, 7 Februari 2017

SOMO: MALAIKA—WATUMISHI WA MAISHA YETU (1)


Furaha Amon

Utangulizi;


Biblia hutaja habari za malaika zaidi ya mara mia tatu. Hata hivyo, watu wengi hawaamini uwepo wao. Isipokuwa katika  siku hizi za karibuni watu wameanza kukubali kwamba kuna viumbe vitakatifu vinavyoweza kuonekana kwa macho.
Ukweli unaonyesha kwamba mara nyingi mkazo wa mafundisho yetu unalenga zaidi kuwafundisha watu juu ya uwepo wa shetani na majeshi yake ya pepo wabaya. Ni muhimu kuwafundisha watu wajue kwamba kama kuna jeshi la pepo wabaya, wajue pia kuna jeshi la Malaika Watakatifu ni vizuri kujifunza na kujua namna ya kuwatumia.
Unapotaka kuandika habari kuhusu Malaika ni ngumu sana kupata msaada kutoka katika maktaba kwa sababu hakuna waandishi walioandika habari za kutosha kuhusu malaika na kwa kweli tunakuwa hatuitendei haki dunia na hasa kizazi kinachokuja. Hebu fikiria jinsi ambavyo barua chache za Mtume Paulo jinsi ambavyo zimesaidia ulimwengu kwa karne nyingi. Kwa hiyo kama tutajifunza na kuwafundisha wengine kuhusu habari za malaika tutakuwa tumeweka misingi muhimu sana kwa watu kuendelea kufuatilia na kushuhudia kuhusu namna ya kupata huduma za mawakili
Akifafanua maono aliyoona kuhusiana na malaika wa Mungu, nabii Danieli aliandika hivi: “Kulikuwa na maelfu elfu [ya malaika] walioendelea kumtumikia [Mungu], na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Danieli 7:10) Mstari huo unaonyesha kusudi la Mungu la kuwaumba malaika. Waliumbwa ili wamtumikie, nao wako tayari kutimiza maagizo yake.

Wakati mwingine Mungu huwatumia malaika kufanya mambo fulani yanayowahusu wanadamu. Katika somo hili nitazungumzia zaidi jinsi anavyowatumia kuwaimarisha na kuwalinda watu wake, kupeleka ujumbe kwa wanadamu, na kutekeleza hukumu yake juu ya waovu.
Nakumbuka siku moja nilipata safari, kwenda katika mji fulani mkubwa. ilikuwa ni safari ya kawaida ambapo niliagizwa kumwakilisha mkuu wangu wa dini, kufanya kazi fulani za kiroho ambazo ilikuwa azifanye yeye. kwa sababu gharama yote ya safari ilichukuliwa na kanisa, na mimi nikaona gharama hii isiende bure nikaona muda huohuo kufundisha semina japo siku tatu, yaani Ijumaa, Jumamosi na nimalizie siku ya jumapili mchana kisha nirudi zangu. kwa hiyo nilikuwa na muda wa kujiandaa kwa ajili ya huduma ambayo nitakwenda kuifanya huko. sikumbuki nilifundisha somo gani! ila nakumbuka usiku mmoja ndio Mungu alinipa neema ya kuwaona viumbe hawa watakatifu, walikuwa wamenizunguka na ninaimba nao wimbo wa kitabuni ambao unaitwa "Ni tabibu wa karibu" kwa kweli ni ngumu sana kuelezea katika maandishi msisimko nilioupata na kutamani kuendelea kuwa nao. Lakini kulikuwa na nuru ya ajabu inamulika kutoka mbinguni huku hao maraika wakishuka na kupanda. kwa kifupi nilimwona Bwana na semina ilikuwa sio ya kawaida. kwa mara ya kwanza ndio niliona kanisa zima wanagalagala chini kwa jinsi Mungu alivyotutembelea.

Malaika Huimarisha na Kulinda
Tangu viumbe hawa wa rohoni waliposhuhudia kuumbwa kwa dunia na Mungu kuwaumba wanadamu wa kwanza, Malaika wameonyesha ushirikiano na kwamba wanapendezwa sana na wanadamu. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu Kristo alisema hivi: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.” (Methali 8:31) Biblia inatuambia kwamba “malaika wanatamani
kuchungulia” mambo yanayomhusu Kristo na mambo ya wakati ujao ambayo yamefunuliwa kwa manabii wa Mungu.—1 Petro 1:11, 12.
Kadiri muda unavyopita, malaika wameona kwamba wanadamu wengi hawamtumikii Muumba wao mwenye upendo. Hilo limewahuzunisha sana malaika waaminifu! Kwa upande mwingine, mtenda-dhambi mmoja anapotubu na kugeuka kumwelekea Yehova, “shangwe hutokea kati ya malaika.” (Luka 15:10) Malaika wanawahangaikia sana wale wanaomtumikia Mungu, na Yehova amewatumia tena na tena kuwaimarisha na kuwalinda watumishi wake waaminifu hapa duniani. (Waebrania 1:14) Fikiria mifano kadhaa.

Malaika wawili walimsaidia Loti na binti zake kuokoka uharibifu kwa kuwatoa nje ya Sodoma na Gomora, yale majiji maovu.* (Mwanzo 19:1, 15-26) Karne nyingi baadaye, ingawa nabii Danieli alitupwa ndani ya shimo la simba, hakuumizwa. Kwa nini? Alisema hivi: “Mungu wangu mwenyewe alimtuma malaika wake na kufunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:22) Malaika walimsaidia Yesu mwanzoni mwa huduma yake duniani. (Marko 1:13) Muda mfupi kabla ya kifo cha Yesu, malaika alimtokea na “akamtia nguvu.” (Luka 22:43) Msaada wa malaika ulimtia Yesu moyo sana hasa wakati huo muhimu maishani mwake! Pia, malaika alimfungua mtume Petro kutoka gerezani.—Matendo 12:6-11.

Je, malaika hutulinda leo? Tukimwabudu Yehova kulingana na Neno lake, tunaweza kuwa na
uhakika kwamba malaika wake wenye nguvu wasioonekana watatulinda. Biblia inaahidi hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.”—Zaburi 34:7.
Hata hivyo, ni lazima tukumbuke kwamba malaika wanamtumikia Mungu wala si wanadamu. (Zaburi 103:20, 21) Wanafuata mwongozo wa Mungu bali si maagizo au maombi ya wanadamu. Hivyo, Yehova Mungu ndiye tunayepaswa kuomba msaada, si malaika. (Mathayo 26:53) Bila shaka, kwa kuwa hatuwaoni malaika, hatuwezi kujua ni kwa kadiri gani Mungu huwatumia kuwasaidia watu katika hali mbalimbali. Lakini tunajua kwamba Yehova ‘huonyesha nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9; Zaburi 91:11) Tuna uhakika kwamba “hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye [Mungu] hutusikia.”—1 Yohana 5:14.

Pia, Maandiko yanatuambia kwamba sala zetu na ibada yetu inapaswa kuelekezwa kwa Mungu peke yake. (Kutoka 20:3-5; Zaburi 5:1, 2; Mathayo 6:9) Malaika waaminifu hututia moyo tufanye hivyo. Kwa mfano, wakati mtume Yohana alipotaka kumwabudu malaika fulani, kiumbe huyo wa roho alimkaripia na kumwambia hivi: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Mwabudu Mungu.”—Ufunuo 19:10.

                   SOMO HILI LITAENDELEA

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni