Ijumaa, 10 Februari 2017

SOMO: ALICHOKIUNGANISHA MUNGU (10)


Huu ndiyo ufunguo wa kulinganisha maneno ya Yesu na ya Musa na ya Paulo. Yesu alikuwa anadhihirisha unafiki wa Mafarisayo tu. Hakuwa anaweka sheria inayozuia kuoa au kuolewa tena. Kama alikuwa anafanya hivyo, basi alipingana na Musa na Paulo, na kusababisha vurugu kwa mamilioni ya watu walioachika, na mamilioni ya watu walioingia kwenye ndoa nyingine. Kama Yesu alikuwa anaweka sheria kuhusu kuoa au kuolewa tena, tuwaambie nini wale ambao wameachika na kuoa au kuolewa tena kabla ya kusikia habari za Sheria ya Yesu? Je, tuwaambie kwamba wanaishi katika mahusiano ya kiasherati? Na, kwa kuwa tunajua Biblia inaonya kwamba hakuna wazinzi au waasherati watakaorithi ufalme wa Mungu (1Wakor. 6:9-10), tuwashauri kwamba waachane na wenzao? Pengine ni sawa, lakini, Mungu si anachukia kuachana?

Je, tuwaambie waachane kitandani mpaka wana ndoa wenzao wa kwanza wafe ili kuwaepusha na zinaa ya kila wakati? Lakini, Paulo si anawakataza wana ndoa kunyimana? Tena, ushauri kama huo si utapelekea watu kujaribiwa kimwili na hata kuamsha hamu za kutaka wana ndoa wenzao wafe?
Je, tuwaambie watu kama hao waachane na wenzao wa sasa na kurudiana na wenzao wa kwanza (kama wengine wanavyosema) – kitu ambacho kinakatazwa na Torati ya Musa katika Kumbukumbu 24:1-4?
Halafu – vipi kuhusu watu walioachana ambao hawajaoa tena? Kama wanaruhusiwa kuoa au kuolewa tena ikiwa wenzao walioachana nao walitenda uzinzi, nani atakayejizatiti kuthibitisha kama kweli uzinzi ulifanyika? Je, itabidi wana ndoa fulani wathibitishe kwamba wenzao walioachana nao walikuwa na hatia ya tamaa tu ili waweze kurudiana? Je, wengine itabidi watafute mashahidi wa kuthibitisha uasherati wa wenzao ili waweze kurudiana?
Kama swali lililopita – vipi kuhusu swala la mwenzi kuzini kwa sababu alikuwa katika ndoa na mtu aliyemnyima tendo la ndoa? Je, ni halali kwa huyo aliyekuwa anamnyima mwenzake tendo la ndoa aruhusiwe kuolewa, na yule mtu aliyezini akatazwe kuoa au kuolewa?
Vipi kuhusu mtu aliyezini kabla ya ndoa? Je, uzinzi wake huo si kukosa uaminifu kwa mwenzi wa baadaye? Je, dhambi hiyo hailingani na uzinzi, kama yeye au mwenzake wangekuwa katika ndoa wakati walipofanya dhambi yao? Mbona huyo aruhusiwe kuoa au kuolewa?

Vipi kuhusu watu wawili wanaokaa pamoja – bila ndoa – halafu wanatengana. Mbona wanaruhusiw akuoa na kuolewa na wengine baada ya kutengana, kwa kuwa hawakuwa na ndoa rasmi? Wana tofauti gani na wale wenye kuachana kisha wakaoa na kuolewa tena?
Vipi kuhusu kweli kwamba “mambo ya zamani yanapita” na “mambo yanakuwa mapya” wakati mtu anapo-okoka (ona 2Wakor. 5:17)? Je, inamaanisha kila dhambi iliyowahi kufanywa isipokuwa dhambi ya kuachana isivyo halali?
Yote hayo na maswali mengine mengi yanaweza kuulizwa, ambayo ni hoja zenye nguvu kabisa kuunga mkono wazo kwamba Yesu hakuwa anaweka sheria mpya kuhusu ndoa. Yesu alikuwa na akili za kutosha kutambua matokeo ya sheria Yake mpya ya ndoa kama ndivyo ilivyokuwa. Hilo tu linatosha kutuambia kwamba alikuwa anaweka wazi unafiki wa Mafarisayo – wanaume wenye tamaa, wanafiki, washika dini, waliokuwa wanaachana na wake zao “kwa sababu yoyote” na kuoa tena.
Sababu ya Yesu kusema kwamba walikuwa “wanazini” badala ya kusema tu kwamba walichokuwa wanafanya ni kosa ni kwa sababu alitaka wao waone kwamba talaka kwa sababu yoyote na kuoa tena baada ya hapo si tofauti na uzinzi, kitu ambacho wao walidai hawafanyi. Je, tuamue kwamba kitu pekee alichojali Yesu ni tendo la ndoa tu katika ndoa ya pili, na kwamba angeunga mkono ndoa ya pili mradi tu watu wasijihusishe katika tendo la ndoa? Hapana. Basi, tusimfanye aseme kitu ambacho hakumaanisha kusema.

MWISHO WA SEHEMU HII

Tutakutana katika sehemu inayofuata ya somo hili Mungu akuinue kwa kufuatilia somo hili.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni