Jumanne, 31 Julai 2012

MAZUNGUMZO YANGU YA MWISHO NA ABEL MOTIKA (MR EBBO)




Kwa watu wanaofuatilia sanaa ya muziki wa kizazi kipya katika ukanda huu wa Afrika Mashariki na kati pamoja na sehemu nyingine mbalimbali duniani na hasa kwa watu wanaopenda kusikiliza nyimbo za kitanzania. Jina hili la “Mr Ebbo” sio jina geni kwao,nasema hili ni jina kubwa kwa sababu nyimbo zake zimechezwa na zinaendelea kuchezwa hata na mashirika makubwa ya utangazaji kama BBC,DW,VOA n.k. lakini ukweli unabaki palepale kwamba watu wengi walimfahamu Mr Abel kupitia picha za video au katika vipindi vya TV vinavyorusha nyimbo zake. Lakini ilikuwa kumuona Abel ana kwa ana akiwa hapa Tanga sio lahisi na unaweza kukaa miaka mingi usimuone kwa macho. Hii  ni kutokana na tabia yake ya kutokukupenda kutembea ovyo mitaani kwa hiyo muda mwingi utamkuta yupo nyumbani kwake ama katika studio yake akitengeneza mashairi ya nyimbo zake ambazo ni tofauti sana na nyimbo za wasanii wengine, na muda mwingi akiwa nyumbani kwake akiangalia filamu za kitanzania ambazo yeye ni mpenzi mkubwa wa filamu hizo.

Nakumbuka ilikuwa kama saa saba mchana nikiwa na rafiki yangu wa kazini Mr Boniface Lyimo tukiwa tumetoka kwenye mapango ya Amboni kikazi nilimuomba tupitie nyumbani kwa Mr Ebbo ambaye nilikuwa nimeahidiana naye kufanya mahojiano kwa ajili ya gazeti la kazini kwetu linaloitwa SAMAWATI. Mimi binafsi nimefahamiana na Mr Ebbo mwaka 1998 wakati bado alikua hajakuwa na jina kubwa katika muziki wa kizazi kipya. Na mimi wakati huo nilikuwa naandaa filamu mojawapo ya Kiswahili inayojulikana kwa jina la KOSA KUBWA ambapo tuliomba kutumia nyumba yake kuigizia baadhi ya vipande vya filamu hiyo.
Kwa ujumla Mr Ebbo naweza kumuelezea kama alikuwa mtu mchangamfu anayeheshimu watu pamoja na kazi zao. Na kama ukienda kwake utatamani usitoke upesi kwa sababu ya uchangamfu na maneno ya utani utani mwingi wa kuchekesha.
Nilipokutana naye wakati natayarisha makala hii pamoja na kwamba tulikuwa na muda mchache sana lakini ulikuwa ni muda ambao ulikuwa wa kurahisha sana na alinipa ushirikiano wa kutosha kabisa.
HISTORIA YAKE KWA KIFUPI
Kwa kifupi nilimuomba anieleze historia yake na alinieleza kama ifuatavyo: Abel Motika alizaliwa 1974 katika Hospital ya Mount Meru Arusha na amesoma elimu ya msingi toka darasa la kwanza hadi la tatu hapo hapo Arusha na baadae akahamia Nairobi ambapo alisoma darasa la nne na la tano ndipo akahamia Tanga kwa wazazi wake, ambapo alimalizia elimu ya msingi na baadae akasoma elimu ya sekondari hapahapa jijini Tanga.

ALIANZA VIPI SHUGHULI ZA MUZIKI?
Kuhusu muziki Abel alisema kwamba alianza kuupenda muziki tangu akiwa mtoto mdogo, na anakumbuka kuwa alikuwa akisikiliza zaidi muziki na hatimaye alijiapiza kwamba ni lazima siku moja atakuja kuwa mwanamuziki. Alipomaliza darasa la saba tu tayari alikuwa amejiunga na kwaya ya kanisa la K.K.K.T usharika wa Kisosora na huko ndiko ndoto yake ilipoingia katika vitendo kwani alijifunza kwa bidii sana misingi ya muziki, pamoja na matumizi ya ala za muziki,mpangilio wa sauti ya kwanza hadi ya nne na mpaka nilipokuwa nikiongea naye aliniambia kwa wakati huo alikuwa na uwezo wa kufundisha watu kupanga sauti na kuziimba na ndivyo alivyokuwa anafanya ukienda kurekodi katika studio yake ya Motika Record Studio ambayo kwa sasa hivi inamilikiwa na mke wake Baby na ameihamishia mjini Arusha ambako ameiboresha zaidi.


Abel alikuwa kwenye kwaya kwa kipindi kirefu na yeye mwenyewe alisema huko ndiko alikojifunza mbinu za muziki,mpangilio wa vyombo sauti pamoja na vitu vingine vingi vya kinidhamu katika sanaa hii ya muziki.
Katika eneo hilo Mr Abel alipenda kuwashukuru sana walimu wake wa kwaya pamoja na watu wote waliomsaidia kujenga kipaji chake katika Muziki na hatimaye kuweza kufanya kazi inayokubalika katika jamii.


ALISEMAJE KUHUSU KUPIGA MUZIKI LIVE ?.
Nilimuuliza Abel ni kwa nini wanamuziki wa Bongo flavor hawapendi kupiga muziki wa wazi (Live) na badala yake wanatumia studio na kupiga nyimbo kwenye maholi kwa mtindo wa kukandamizia kupitia kwenye CD walizotengeneza studio? na nilimuuliza kwamba haoni hatari za kupoteza hamasa ya watu kujifunza vyombo au ala za muziki iwapo jamii itaendekeza mtindo wa kutengeneza muziki studio na kuacha kupiga muziki live?
Abel alisema inawezekana watu wengi wakaamini hivyo na hasa wanamuziki na wapenzi wa muziki wa zamani. Lakini yeye kwa maoni yake kama mwanamuziki wa kizazi kipya haoni ubaya wa kutengeneza muziki studio kwa sababu ni kazi yenye gharama nafuu na inayohitaji watu wachache kufanya kazi ya watu wengi kwa ubora  uleule au na kuzidi pia.Anasema binadamu kila siku amekuwa akiumiza kichwa na anabuni mbinu za kurahisisha maisha na ndio maendeleo yenyewe kwani maendeleo ni mabadiliko.
Alisema hata magari ya zamani yalitengenezwa na mfumo wa gia za manual,lakini wataalamu wamegundua magari ya mfumo mpya wa gia wa automatic ambayo ni rahisi zaidi kuyaendesha na sasa hivi mengi yanakuja nchini kwetu inawezekana baada ya muda tusiweze kuyaona tena magari yenye mfumo wa gia wa manual yakiingia sokoni kwani sasa hivi kuna mabasi na magari makubwa  malori yanayotumia mfumo wa gia wa Automatic. Kwa hiyo kama ilivyo kwenye magari hata na kwenye muziki ni hivyo hivyo.

Abel anaamini kwamba muziki live utaendelea kuwepo na utakuwa na wapenzi wake lakini pia na muziki wa studio utaendelea kuwepo na utakuwa na wapenzi wake na wote utaendelea kuwepo kama vile ambavyo sasa hivi kuna magari yenye mfumo wa gia wa manual na automatic yameendelea kuwepo na watu wamekuwa wakitumia kwa kadri wanavyopenda wapo wanaopendelea yenye mfumo wa manual lakini pia wapo wanaopendelea yenye mfumo wa automatic.


Abel aliamini kwamba hata kwenye muziki utakuwepo muziki live ambao utakuwa na wapenzi wake na utaendelea kuwepo lakini pia utakuwepo muziki wa kutengenezwa studio ambao pia utakuwa na wapenzi wake upo ambao ukiwapeleka kwenye muziki live hawatakuelewa. Alisema kwamba muziki kama vile muziki wa reggae na jazz ni aina ya miziki inayopendeza zaidi ikipigwa live kuliko miziki ya Pop na RnB

Abel aliamini kwamba muziki wa studio hauwezi kuua vipaji vya watu wenye nia ya kujifunza vyombo vya muziki kama watakuwepo.Kwani fursa zitaendelea kuwepo kwa watu wanye nia ya kujifunza, lakini hapendi watu walazimishwe kurudi nyuma kimaendeleo au kuogopa kutumia teknolojia mpya kwa hofu ya kuua vipaji kwa sababu hata huko kwenye teknolojia mpya pia kutahitaji vipaji ndio maana pamaja na kuwa na teknolojia mpya lakini sio kila mtu ndio sasa anaweza kufanya kazi ya muziki au kuwa mwanamuziki.
KWA NINI KUMEKUWA NA TEKNOLOJIA YA KISASA KATIKA MUZIKI.?
nilimuuliza Ebbo swali hili nay eye alinijibu kwamba Teknolojia inakuja kwa lengo na makusudi ya kupunguza ugumu wa kazi na gharama. Hivyo watu wanapotumia akili ya kuvumbua vitu ni muhimu kuvitumia ili kuheshimu mawazo yao. Kabla watu hawajavumbua magari yanayokwenda kwa injini ya mvuke wa mafuta waliwakuta wenzao wanatumia magari yanayokokotwa na wanyama. Kwa maana hiyo na sisi hatuwezi kuwalazimisha watu kutembea na punda kama zama za mawe wakati sasa hivi kuna vyombo vyenye kasi kubwa ya kurahisisha safari,tukifanya hivyo tutakuwa wapinga maendeleo na wasaliti wa utandawazi na tiknolojia.
Kwa hiyo Abel anasema kwamba sio vizuri kuwalazimisha watu wapende muziki live wakati sio kila mtu anayependa muziki uwe live wapo watu katika kizazi hiki ambao hawajawahi kwenda kwenye tamasha linalopiga muziki live na hata ukimpeleka atashangaa




NI NINI SIRI YA NYIMBO ZA MR EBBO KUKUBALIKA
Nilimuuliza Abel ni kwa nini nyimbo zake zinakubalika na zinapendwa na kada ya watu wa rika na hadhi tofauti. Abel alinijibu kwamba Tangu zamani alijiwekea misingi ya aina ya nyimbo alizotaka kuziimba. Alipenda  aimbe nyimbo ambazo hazitamkwaza mtu, Nyimbo zenye aina ya ujumbe unaowakilishwa kama ucheshi lakini ambao ndani yake kuna ujumbe utakaomfanya mtu afikiri. Alisema  kuwa kama angekuwa anapenda kuimba nyimbo za mapenzi au za kisiasa pengine kila siku angekuwa anatoa nyimbo. Lakini nyimbo anazotunga yeye ni za aina yake tofauti na za mtu mwingine kwa sababu  hazimkwazi mkubwa,mtoto,mwanamke,mwanamume kijana mzee na zinapendwa hata na watumishi wa Mungu. Aliniambia kuna   wachungaji na mashehe wanazifurahia nyimbo zake na kumueleza waziwazi kuwa wanaikubali sana kazi yake. Hii ni kwa sababu ya aina ya tungo zake alisema Mr Ebbo kuwa anatengeneza nyimbo zenye ujumbe unaoleweka, na video zake anajitahidi ziwe safi ambazo hazitasababisha wazazi wakimbiane na watoto sebuleni,hiyo ndio siri kubwa ya mafanikio yake katika sanaa hii. Anasema yeye kama hajapata wazo la kuimba anaona ni bora atulie kuliko kulazimisha kutoa nyimbo ili kuwahi soko na hili ndilo tatizo kubwa linalowapata waimbaji wengi wa muziki wa kizazi kipya.

NI MWANAMUZIKI GANI AMBAYE EBBO ALIYEMPENDA?
Nilimuuliza Mr Ebbo ni mwanamuziki gani anayempenda na ambaye angependa awe kielelezo chake katika mafanikio yake kimuziki. Alinijibu kuwa ni mwanamuziki wa zamani wa Jamaika Robert Nesta Marley (Bob Marley). huyu ni mwimbaji ambaye ndio aliyempenda na kumfanya kuwa kielelezo chake katika muziki tangu zamani. Abel alisema kwamba yeye ni mpenzi wa muziki wa reggae na alipenda sana kufanya muziki wa reggae lakini kulingana na soko la muziki kwa nchi yetu ingekuwa ni vigumu sana kwake kupata mafanikio aliyokuwa ameyapata kama angepiga muziki wa reggae. Lakini alikiri kwamba ameamua kupiga muziki anaopiga sasa ili kuwashika watu wanaomkubali lakini muda mwingi akiwa nyumbani nyimbo kwake nyimbo nyingi anazosikiliza ni za reggae


   
NI WANAMUZIKI GANI WA TANZANIA WANAOMVUTIA?
Baada ya kunijibu aina ya muziki na wanamuziki anaowapenda katika dunia nilimgeuzia kibao aniambie wanamuziki anaowapenda Katika nchi yetu ya Tanzania nay eye alinijibu kuwa  anapenda sana wanamuziki wote ambao wapo makini na wanaoheshimu muziki kama taaluma na sio sehemu ya kupotezea muda au kujifurahisha na kuwafurahisha watu tu.  Anapenda  wanamuziki wote wanaojua kwamba muziki ni kazi inayohitaji staha na kujiheshimu kama ofisa au mwakilishi wa wananchi.
Lakini bado nilijitahidi sana kumbana aniambie mwanamuziki mtanzania ambaye yupo ndani ya uvungu wa moyo wake ndipo aliponifichulia kwamba  anavutiwa sana na kazi inayofanywa na Msanii Mrisho Mpoto na Saida Kaloli. Anasema kwamba Mpoto anapenda sana muziki wake kwa sababu ni muziki wa  kufunga na sio wa kuimba mambo waziwazi alisema katika wimbo wake mpya ambao aliamini kuwa ungetoka  karibuni alitegemea kuwa utakuwa na fikra mpya. Na atajaribu kuwakumbusha Watanzania na hasa wakazi wa Tanga kwamba pamoja na kuwepo kila kitu katika Super Market lakini wasisahau walikotoka wakumbuke na masoko yao ya ngamiani mgandini na masoko mengine ya mitaani ikiwa ni pamoja na magenge. Alisema vitu kama super market sio utamaduni wetu kwa asili ni utamaduni wa Ulaya hivyo tusiuuwe utamaduni wetu na kuukumbatia utamaduni wa Ulaya.
Anasema popote uendapo katika dunia hii kitu cha kujivunia ni cha kwako. na usipende kujivunia cha mtu mwingine. Abel ambaye mpaka wakati naongea naye tayari ana Albam kadhaa. Alisema  kwamba wimbo ambao anauheshimu ni ule uliomtambulisha kwenye ramani ya muziki wa Tanzania wimbo wake wa  kwanza “mimi maasai  bwana”ambao ulikuja kubeba na nyimbo nyingine nyingi.
Abel ambaye ni baba wa watoto watatu hakutaka kabisa kuongelea suala la mgogoro wa ndoa yake na mzazi mwenzake ambayo ililipotiwa sana kwenye vyombo vya habari na hasa magazeti ya udaku yaliyotoka kila wiki. Nilimuuliza kama anaweza kutoa ufafanuzi kwa mashabiki na wapenzi wake wajue ni nini hasa kilichotokea?

Abel aliniambia kwamba anayaacha yaliyoandikwa yabaki kama yalivyo kwa sababu ni mambo ambayo yanaigusa sana nafsi yake na hawezi kusema neno baya lolote kwa sababu yule ni mzazi mwenzake na ndugu yake kwa maana wanaunganishwa na watoto kwa hiyo akimsema vibaya au akimtukana ni kama anajitukana yeye mwenyewe.
Baada ya mazungumzo haya sikuwahi kumuona tena Ebbo na wala sikusikia habari zake mpaka wakati naandaa shindano la kusaka vipaji. Nilimuweka katika orodha ya watu watakaotembelea kambi yatu ya washiriki. Lakini siku moja alfajiri sana nilipigiwa simu ya kunitaarifu kwamba Ebbo ameaga dunia. Na mtu aliyenipa taarifa hizo namheshimu sana lakini nilifikiri labda taarifa zake sio sahihi lakini baada ya muda nikanza kupata simu za watu mbalimbali ikawa ni habari mbaya sana iliyofunika jiji la Tanga nasi tukasema Jina la Bwana litukuzwe
Huyu ndio MR EBBO mwanamuziki,rafiki,shujaa wetu aliyetufurahisha wakazi wa jiji la Tanga na watanzania wote kwa ujumla.
Mke wamarehemu Ebbo akiwa na dada wa marehemu Ebbo


wazazi wa Mr Ebbo siku ya mazishi ya mtoto wao.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni