Jumamosi, 4 Agosti 2012

MWENDO WA KANISA ZAMA ZA UTANDAWAZI. SEHEMU YA KWANZA









Dunia inapita katika kipindi cha mabadiliko makubwa Sana katika Nyanja ya sayansi na teknolojia. Kasi ambayo dunia inakwenda ni kubwa sana kuliko tunavyofikiri, Na inagusa karibu katika nyanja zote za maisha ya kila siku ya binadamu ikiwemo hata na ndani ya kanisa. 

Biblia inaposema kwamba katika nyakati za mwisho maarifa ya wanadamu yataongezeka,watu wengi hudhani kwamba kanisa halitahusika na mabadiliko hayo lakini ukweli ni kwamba kanisa ni mdau wa mabadiliko na kamwe haliwezi kujitenga na mabadiliko yanayotokea duniani kisayansi,kiutamaduni,kijamii n.k.
Mara nyingine wakati nchi yetu ambayo iko katika kundi la nchi zilizoko katika dunia ya tatu inapojiandaa kuingia katika mabadiliko fulani ambayo nchi zilizoendelea na zinazoendelea imefikia, inakuta dunia ya kwanza na ya pili zimeshahama huko na kwenda hatua ya mbali zaidi. Hali hii imesababisha kanisa kuburuzwa na 
mabadiliko haya na kuwa kama mchezaji mlalamishi katika uwanja wenye mabadiliko ya sheria na kanuni za mchezo wa maisha katika jamii. Wenzetu walioipigania injili walijitahidi sana kujaribu kupingana na mabadiliko haya yasiingie ndani ya kanisa lakini walishindwa hii ni kwa sababu waliotuletea dini hizi walileta bia na utamaduni wao ambao wao wanauita ustaarabu na ndio maana dini za kikrito waliotuletea dini hii walitoka ulaya na ndio waliotuletea ustaarabu wa kuvaa suruali na mashati na wakati unahubiri ni vizuri uvae koti japo na tai tofauti na walioleta dini ya kiislamu ambao wanatoka mashariki ya kati na ambao vazi lao la heshima 
ni kanzu na vinginevyo hawakuelewi. Mtumishi mmoja aliniambia kwamba zamani ilikuwa ni marufuku hata kutumia gitaa kwenye ibada, ile kukubali tu kutumia magitali ndani ya kanisa lao ilikuwa ni mjadala mgumu sana na hata ilipokubaliwa walikuwa na aina ya mapigo waliyotakiwa kupiga. siku moja walipiga wimbo mmoja kwa mtindo wa regae ya Jamaika ambayo kwa wakati huo ilikuwa inavuma sana miaka hiyo ya 1970. Baada ya ibada kwisha kwaya nzima walisimamishwa na wengine wakatengwa. Lakini siku hizi hakuna kitu kama hicho na kanisa kama halina magitaa watu ni vigumu sana kuhisi kama kweli wameabudu. Hapo tunaweza kusema utandawazi umeingia mpaka kanisani
.
Wengine walijaribu kuzuia kwa kufunga na kuomba ili kwamba matumizi ya internet yasiingie Tanzania na hata yakiingia yasiguse kanisani wakiamini kabisa kwamba ni mtandao wa mping Krito lakini haikuwezekana hatimaye yaliingia na hatimaye wao wenyewe siku hizi wanayatumia na wanaona yana faida kubwa sana katika kazi ya Mungu na makanisa ambayo hayatumii mtandao yanajirudisha nyuma na kujiweka katika wakati mgumu kupambana na mazingira yanayobadilika kila kunapokucha.
Sasa hivi wataalamu wanafikiria kutengeneza memory card kama zinazotumika kwenye simu kwa ajili ya kuweka na kupata taarifa za  binadamu ambazo zitachomekwa ndani ya miili ya watu,kama vile walivyokuwa wanapandikiza vijiti katika uzazi wa mpango ambavyo
Vitawawezesha kila mtu anaposafiri hakutakuwa na haja ya kuchukua pasiport  ila kutakuwa na mashine maalumu mipakani,kwenye viwanja vya ndege na kwenye ofisi za uhamiaji ambazo mtu akipita zitasoma taarifa na kumbukumbu zake zote.

Haya ndio maandalizi ya kuifanya dunia kuwa kijiji kimoja, na kuivunjilia mbali kabisa mipaka ya mataifa. Jambo hili Biblia ilishaliona na kwa kweli halikwepeki tutake ama tusitake ni lazima hatimaye dunia itakuwa na kiongozi mmoja. Na tutatumia sarafu moja na watu hawataulizana juu ya utaifa wa mtu, haya mabadiliko tunayoyaona ya jumuiya za kikanda kama SADC, ECOWAS n.k. ni maandalizi ya huko tunakoelekea

UTANDAWAZI NINI MAANA YAKE NA UNA NIA GANI.

Nia kubwa ya utandawazi ni kuvunjilia mbali mipaka ya nchi na kuifanya dunia hatimaye kuwa kama kijiji kimoja katika nyanja za elimu, mawasiliano, sayansi na Teknolojia.
Tangu zama za mawe dunia imekuwa ikipita katika mabadiliko mbalimbali yenye lengo la kumsaidia mwanadamu na kumrahisishia kukabiliana na maisha yake katika mazingira yake. Mtoto mmoja wa kizungu alimwambia mtoto mwenzake wa kiafrika ambaye alimuona akihangaika kujumlisha mahesabu kwa kuandika akiona aibu kutumia kikokoteo cha hesabu (Caluculator) akamwambia sasa babu zetu walihangaikia nini kubuni chombo hiki kama hutaki kukitumia, ilikuwa ni wajibu wao kuturahisishia sisi maisha ili na sisi tuwarahisihie watoto wetu maisha. Na hii nikweli tunajua kwamba binadamu alianza kusafiri kwa miguu, punda wenye

mikokoteni Na kila siku watu wamekuwa wakibuni vitu mbalimbali kwa lengo la kurahisisha maisha ya mwanadamu, ndio maana tunaweza kusema kwamba wale watu waliotajirika sana duniani ni wale waliobuni vitu ambavyo vilikuja kuwasaidia sana wanadamu kutatua matatizo yao, fikilia kwa mfano mtu aliyevumbua vyombo vya usafiri kama vile gari, ndege n.k.

DUNIA KATIKA MABADILIKO MAKUBWA
Katika karne ya 21 dunia iliingia katika mabadiliko makubwa Sana pamoja na kwamba watu wengi walihisi kwamba kompyuta zingeshindwa kuusoma mwaka 2000 kwa sababu mwaka huo haukuingizwa kwenye kompyuta lakini wataalamu wakabuni kitu kilichojulikana kama Y2K ili kuendeleza na kubuni mambo mengine makubwa zaidi ambayo kwa kiasi kikubwa yameleta mabadiliko makubwa katika ulmwengu wa sayansi kwa lengo la kumsaidia mwanadamu kukabiliana na maisha yake.
Tangu wakati huo teknolojia ya habari na mawasiliano (Teknohama) imekuwa ni muhimili mkubwa sana unaobeba mabadiliko haya. Wakati Biblia inatoa tahadhali kwamba katika nyakati za mwisho maarifa ya wanadamu yataongezeka Sana, watu waliookoka ndani ya makanisa wanadhani kwamba andiko hilo haliwahusu wao bali linawahusu watu wa dunia. Matokeo  yake kanisa linajikuta linaburuzwa na mabadiliko ya dunia bila kuwa na maandalizi ya kimkakati ili kupambana na mabadiliko yanayoletwa na sayansi na teknolojia kwa sababu hayana budi kuja na ni lazima yaje. Paulo mtumishi wa Mungu aliwahi kuwaeleza wakorintho kwamba alipowaambia wajitenge na dunia, hakuwa na maana kwamba waondoke kabisa hapa duniani. Bali aliwataka wajitenge na tabia za kidunia.

TUNAWEZAJE KUJITENGANISHA NA TABIA ZA KIDUNIA?


Lakini kwa hali yoyote ile ni vigumu sana kuwatenganisha watu wanaoishi hapa duniani na watu waliopo kanisani kwa sababu watu waliopo kanisani ni zao la jamii ya watu waliopo katika mazingira hayo na kwa uhakika  ni haohao, isipokuwa wakiingia kanisani kuna mafunzo wanayoyapata  mafunzo yanayohusu namna ya kumjua Mungu na thamani ya wokovu na hali halisi ya maisha ya dunia  inavyokwenda, kwa ujumla hakuna namna ya kujiepusha na mabadiliko ya hali ya dunia kwa sababu hakuna sehemu inayoweza kusalimika au kuepuka mabadiliko haya kwa sababu hiyo ni muhimu kuweka mikakati ya kueleweka bila ya hivyo kanisa linaweza kujikuta linaingia katika mabishano ya vitu vidogovidogo kama mitindo ya mavazi,mapambo ya akina mama na nywele mitindo inayoletwa na mabadiliko ya nyakati, kama tunavyoona mambo yanayoendelea hivi sasa wakati nguvu kubwa ya fedha inatumika kununua vipindi kwenye Televisheni kwa nia ya mabishano ambayo hayana faida yoyote kwa kukuza kazi ya Mungu.

MTINDO WA KUWAZUWIA NA KUWAFUKUZA WATU KANISANI

Hakuna mwanadamu aliyekufa kwa ajili ya dhambi za wanadamu na kanisa ni mali ya Bwana Yesu ni makosa kumfukuza mtu kanisani wakati aliyemfia bado anamuhitaji.


Makanisa Mengine yamefikia hatua ya kuwazuwia au kuwafukuza watu kuingia kanisani. Cha kusikitisha zaidi ni kwamba watu hao ni jamii ya watu ambao bado hawajaamini ambao wamewasindikiza ndugu zao kwenda kwenye maombezi kanisani. Lakini wakifika milangoni wanakuta kuna watu wamewekwa na kanisa kwa nia ya kuwakagua na wakiwaona labda wamevaa au wametengeneza nywele saluni, basi wanawalazimisha wafunge vilemba au wavae kanga na magauni marefu. 

Ukifikiria  sana utaona kwamba hapo kuna tatizo kubwa sana na kuna maswali mengi sana ya kujiuliza na swali la muhimu sana hapo ni kuuliza ni jukumu la nani? Kumsaidia mtu huyu aweze Kubadilika na kuwa mtu mwenye kiwango cha kufaa kuingia katika majengo ya kanisa lenu?.

KANISA NI MFANO WA MASHINE YA KUSAGA
Mtu anapokwenda mashine kusaga nafaka ili kupata unga akiwa mashine ataona vitu vitatu muhimu. Kwanza ataona kinu hii ni sehemu ambayo ukifika mashine unaweka nafaka na mara nyingi kuna mtu anayekuwa pale kuhakikisha zile nafaka zote zinakwenda kwenye mkondo unaotakiwa na kuzielekeza kwenda sehemu ya pili ambayo ni kwenye mashine yenyewe mortal. Kazi ya mortal ni kuisaga nafaka hii ili iwe unga na kisha ataona kitu cha  tatu ambacho mara nyingi huwa ni mfano wa bomba ambalo limezungushiwa kitambaa cheupe na sehemu hii ndiko unakotokea unga safi uliotokana na nafaka iliyosagwa na mortal. Kwa maana hiyo, kama itatokea nafaka ambayo haikusagwa basi ujue kwamba haikupita katika mortal kwa mfano huu ni kwamba watu wa dunia ni mavuno (nafaka).




Wakristo waliookoka ni sawa na watenda kazi ya kwenda shamba na (kuvuna watu wa dunia na kuwapeleka kwenye kanisa) kuleta nafaka mashine. Wakifika mashine kuna mtu wanayemkabidhi nafaka hizo ili aziweke kwenye kinu, tayari kwa kuzisaga kuwa unga ambapo kwa mfano huu kinu ni kanisa la Mungu ambapo watenda kazi (washirika wa kanisa) kazi yao ni kuleta nafaka mashine na wakifika hapo mashine kuna mtu (Mchungaji), yupo hapo kwa ajili kuziongoza hizo nafaka kuelekea kwenye mortal (Roho Mtakatifu). Kwa hali yoyote nafaka zikifika kwenye kinu haziwezi kubadilika na kuwa unga bila kupita kwenye mortal ambayo ni mafundisho na maisha ya kiroho yanayoletwa na Roho Mtakatifu, na kumbadilisha mtu taratibu hatua kwa hatua.
Kwa kutokulijua hili au kwa ghiliba za shetani, watenda kazi wasiokuwa na ujuzi wa vita vya kiroho badala ya kufurahia na kushukuru Mungu kwamba mavuno yamekuja yenyewe kwenye kinu bila kuyafuatilia. Badala ya kutulia na hao watu na kuwaelekeza kwenye kinu kwa upole na upendo mwingi.

Wao wanataka watu hao wageuke unga ghafla bila kupitia kwenye mortal kitu ambacho kwa kweli hakiwezekani. Nafaka ikiwa kwenye kinu hata ukemee mpaka Mapovu ya damu yakutoke, Nafaka bila kupita kwenye mortal haiwezi kugeuka na kuwa unga. Hata kama ukikemea na kuomba mpaka siku Yesu akirudi punje ya nafaka itabaki kuwa punje, ni mpaka utakapofuata kanuni za Mungu, kwa sababu ni Mungu anayetupa mabadiliko ya kweli katika wokovu. Inawezekana yule anayewazuwia watu wasiingie kanisani wakati watu wanaotaka kukutana na Mungu wao aliyewanunua kwa damu yake ya thamani. halafu yeye anawazuwia kana kwamba yeye aliokolewa kwa sababu alikuwa mtakatifu sana. Mtu huyo nina mashaka naye sana kama sio wakala wa shetani, basi hajui anachokifanya na ama hajui sababu ya kifo cha Bwana Yesu pale kalvary.

KILA MTU KANISANI NI MUHIMU NA ANAFAA KWA MUNGU.
Inawezekana mtu huyo akawa sio muhimu kwako wala kwa kanisa lako lakini mbele za Mungu ni mtu muhimu sana na anajulikana sana kwenye ufalme wa mbinguni.

Wakati fulani nilikwenda kutembelea kanisa moja nje kidogo ya Mji wetu, na baada ya kumaliza kufanya huduma, Mchungaji wa kanisa lile akaniongoza ofisini kwake kwa Mapumziko na mazungumzo mafupi.
Wakati tunaendelea na mazungumzo hayo aliingia ofisini mshirika mmoja wa kike kwa shughuli za kiutumishi, na baadae alipotoka nje ya ofisi mchungaji alitaka kupata mawazo yangu na maoni yangu kuhusiana na muonekano na hasa mavazi aliyokuwa amevaa yule mwanadada.
Kwanza sikuelewa mchungaji anataka kusema nini juu yake, hata hivyo nilikuwa naamini kuna kitu anataka kunifundisha kutokana na swali hilo hivyo ilinibidi niwe makini kueleza jinsi ninavyomuona kwa hisia zangu mwenyewe. Nikamwambia mchungaji huyu dada amevaa vizuri sana na ningependa wakina dada wote makanisani mwetu wavae mavazi ya heshima kama aliyovaa yule dada, kwanza ni mavazi ya kisasa na unaweza ukaingia nayo mahali popote kwenye hadhi kubwa.

Nikaona mchungaji anacheka kisha akaniambia alitegemea majibu kama hayo kutoka kwangu ila akaniambia kuna kitu kikubwa sana ambacho yeye binafsi Mungu amemfundisha kupitia katika maisha ya yule dada. Akasema huyu dada alikutana na Bwana Yesu akiwa kwenye shughuli za ukahaba changudoa akiwa kwenye danguro (sehemu ambako watu wanajiuza miili yao) na alikutana na Bwana Yesu akiwa huko na akamuongoza kuja katika kanisa hili analolichunga na yeye akampokea. Anasema kama unavyofahamu, Maisha ya watu wa aina hii hakuwa na nguo ya maana hata moja.
Nguo zake nyingi zilikuwa ni zile alizokuwa anazivaa kwenye shughuli zake za kujitafutia riziki kwa njia haramu. Anasema alipofika kanisani washirika hawakumkubali na wengine walikuwa wakimtolea maneno ya kashfa kwamba anawadhalilisha, wengine walitaka aondoke kabisa kanisani.
Hili jambo ni lazima watu walifahamu kwamba kanisa ni mali ya Yesu mwenyewe na yeye ndiye anayejua nani ampeleke katika kanisa gani, si jukumu letu kulalamika kwamba mbona kanisa ninalolichunga halina matajiri au wafanyakazi wenye hadhi kubwa (waheshimiwa) kanisa lipo kwa ajili ya watu wote.  

Dunia ni kama bahari iliyochafuka na kanisa ni kama meli ya usalama iliyoko juu ya bahari. Watu wanapookoka inakuwa ni sawa na watu waliozama baharini wanategemea wakiokolewa na kuingia kwenye Meli (kanisa) watakuwa salama na watafundishwa namna ya kuishi kwenye meli hiyo. Sasa hawawezi kujifunza kwa siku moja au mbili wengine inaweza kuwachukua miaka kadhaa kuweza kujua namna ya kuishi katika chombo hicho (kanisa) Mchungaji yule anasema mara nyingi yule dada alikuwa anakwenda ofisini kwake akiwa analia na kueleza jinsi ambavyo anabaguliwa na kusemwa vibaya na washirika wenzake ndani ya kanisa.
Mchungaji alimwambia kwamba wala asisikilize neno la mtu awaye yeyote kuhusu kitu chochote kama kuna kitu kibaya yeye mchungaji ndio atamwambia. Kwa maana yeye ndio mchungaji wake. Maneno yale yalikuwa yanamfariji sana yule dada na kumpa bidii ya kuhudhuria vipindi karibu vyote vya kanisani. Baadae alianza kubadilika na akawa anavaa vizuri kushinda hata wale waliokuwa wanataka kumfukuza kanisani.  na kwa kweli ni mtu anayempenda sana Bwana Yesu na hata wakati huo alikuwa ni msaada mkubwa sana kwa mchungaji wake na kanisa lake kwa ujumla.
Muda mwingi Yule dada anautumia kanisani kwa kuombea watu wanaofika kanisani na kufanya usafi wa kanisa.

Hii ilikuwa ni habari ya ajabu sana kuhusu nguvu ya Roho mtakatifu inavyoweza kumbadilisha mtu kutoka katika shimo la giza na kumfanya kuwa nuru na kielelezo kwa wengine. Mchungaji anasema katika mafundisho aliyokuwa akipewa na Mungu kwa ajili ya kanisa kwa kipindi chote cha mabadiliko ya yule dada hakukuwa na mafundisho kabisa yanayohusu mavazi au mabadiliko ya tabia, mafundisho mengi yalihusu imani na nguvu za Mungu.

Bwana ndiye mchungaji wangu sitapungukiwa na kitu.

Nimekupa ushuhuda huu makusudi ili uweze kufahamu kwamba
Imani huwa inazaliwa na imani huwa inakuwa ama inaongezeka kulingana na jinsi ambavyo unavyojitoa mbele ya Mungu, na jinsi vile Mungu anavyoonekana kwako. Kwa sababu imani ni mchakato na maisha ya wokovu ni kuzaliwa mara ya pili haitawezekana mtoto  akazaliwa mara moja akaanza kuongea na kutembea ni lazima tufahamu kwamba, mtoto kabla hajakuwa mtu mzima kuna hatua nyingi anazopitia na anahitaji uangalizi wa hali ya juu sana . Kuna makosa mengine mtoto akifanya wala huwezi kumlaumu bali utawalaumu walezi wake au wasimamizi wake, lakini kuna kipindi ambacho mtoto anapoendelea kukua inabidi kumwelekeza kwa bidii juu ya nini anachotakiwa kukifanya na kipi hatakiwi kukifanya na kuna kipindi kinapofika huna haja tena ya kumwelekeza mtoto nini cha kufanya hapo ndipo utakapoweza kumuadhibu lakini inapotokea mtoto amezaliwa tu na wewe unaanza kumchapa hata kabla hajajua maisha yanakwenda vipi. Ukifanya hivyo wewe mzazi watu watakulaumu na ikibidi serikali itakupokonya mtoto huyo alelewe na mtu mwingine. Maana wewe utamuua mtoto (kwa maana wewe hujui kulea kuna kumwogesha kumnawisha akijichavua na kumtunza kwa upendo,kama kuna mchungaji hajui jambo hili basi ni hatari kwamba imani yetu itakuwa imevamiwa kwa kiasi cha kutisha sana au huyo

mchungaji atakuwa ama amechukua washirika kutoka kwa wachungaji wengine au labda anachunga malaika kutoka mbinguni lakini kama ni wanadamu wa kizazi cha leo ni lazima awe mpole na afanye kazi ya Mungu kwa uvumilivu sana, kitendo chochote cha kumfukuza mshirika ama kumzuwia kuingia katika jengo la dini yako ni kukwepa wajibu wa kiutumishi, kwa sababu watu hawawezi kufanana na unaweza ukamuona wewe mtu Fulani hafai na matokeo yake akaja kuwa mtenda kazi hodari kabisa nyumbani kwa Mungu na akawa msaada mkubwa kwa ufame wa Mungu na ukashangaa kabisa, haya mambo yameshatokea sana kwa watumishi wengi waliwafukuza watu na baadae wakaja kugundua kuwa ama hawakushauriwa vizuri au hawakutulia vizuri kumsikiliza Mungu. Maisha ya Kiroho Sio Mepesi Kama Tunavyofikiri.

TUNAPAMBANA NA SHETANI YULEYULE WA KWENYE BUSTANI YA EDEN LAKINI KATIKA MAZINGIRA YALIYOBADILIKA SANA.
Ni muhimu sana kufahamu kwamba tunapambana na shetani yuleyule aliyemuangusha Adamu na mkewe Eva katika bustani ya eden lakini tunapambana naye katika mazingira yaliyobadilika sana. Na ni lazima na sisi tuhakikishe kwamba tunakwenda na kubadilisha mbinu mara kwa mara ili kukabiliana na dunia inayobadilika kwa kasi kubwa.



Kama kijidudu cha maralia tumekibadilishia dawa mara nyingi sana, lakini bado kijidudu hiki kimeendelea kuua watu wengi zaidi kuliko ugonjwa wa aina yeyote na kwa kweli dawa yake halisi ni quinen. Lakini tumekibadilishia dawa za aina mbalimbali kama vile cloloquine maralaquin shelaquin n.k. na kama unavyoona katika kila dawa ilipobadilishwa qunine ilikuwepo ndani yake.
Hapo ina maana kwamba kila walipokuwa wakitibu kijidudu hiki kiliporudi kilikuja kikiwa kimejiimarisha zaidi na kujikinga ili kuzuwia Quinen isikipate, pengine kiliweka gamba gumu na kufumba mdomo wake. Matokeo yake dawa inaonekana haifai.
Hapo inabidi itafutwe dawa ambayo kwanza itakwenda kuvunja lile gamba na kisha itakibana mdomo kile kijidudu na ndipo Quinen itapitapenya na kukipata kile kijidudu na kukiua. Ndio maana siku hizi kuna dawa mseto ya maralia maana yake ni mchanganyiko wa dawa zaidi ya moja hii ndio maana ya neon mseto.
Nimetoa mfano huu kukuonyesha kwamba kama kijidudu kidogo cha maralia kimetusumbua na tumekibadilishia dawa mara nyingi kiasi hicho nab ado kinatusumbua je itakuwaje kwa shetani. Ni wazi kwamba hatuwezi kupambana na shetani kwa staili ileile iliyotumika kwa mfano miaka kumi tu iliyopita.
Kwa wale watu wa siku nyingi kidogo watakumbuka kwamba baada ya kupata uhuru nchi yetu iliamua kufuata mfumo wa siasa ya ujamaa na kujitegemea ambayo ilimlazimisha kila mwenye uwezo wa kufanya kazi anafanya kazi na wakati huohuo serikali ilijitahidi kuhakikisha huduma zote muhimu na za msingi watu wanazipata bure kwa hiyo watu waliishi kijaa zaidi.
Kwa sababu hiyo hakukuwa na wizi kabisa, katika nyumba zingine watu waliweka pazia tu wala wezi hawakuiba,lakini baadae baada ya kutoka kwenye misingi ile ya ujamaa ambayo ilijali zaidi utu wa mtu na kuingia katika siasa zinazochanganyikana na ubinafsi watu walianza wizi,ilibidi watu wabadilishe na waanze kutengeneza milango mingine ya mabati na baadae milango ya mbao. Lakini wezi nao walikuwa wanabadilisha mbinu na kuvunja milango ya mbao kwa kutumia mawe makubwa yanayowekwa kwenye magunia na kurushwa kwa nguvu kwenye milango ya mbao na kuivunjilia mbali. Mawe haya wanayaita jina la “fatuma.”
Siku hizi watu wanajenga majumba makubwa yenye milango ya chuma na walinzi wenye bunduki na majibwa wakali lakini bado wezi wanaiba. Mlinzi analeweshwa au ananyongwa,mbwa wanapewa maini ya sumu na wezi wanakuja na gesi ya kukatia vyuma wanaingia na kuharibu
Tena katika hali nyingine ni afadhali nyumba yako uweke vitasa kuliko kuweka kufuli maana ukiweka kufuli ni sawa na kuweka tangazo kwamba mwenye nyumba hii hayupo.
Mifano hii miwili ingawa inaweza kuwepo na mingine mingi ambayo itatusaidia kufahamu kwamba mbinu zinabadilika kulingana na hali na nyakati.
Tukumbuke kwamba kila nyakati zina watu wake na stahili zao za maisha, wakati Yohana mbatizaji analeta injili kwa watu wa kizazi chake walimpokea na walimkubali kwa staili aliyoingia nayo ya kuvaa mavazi ya ngozi na kula asali na matunda watu walimuelewa na walitubu. Lakini  wewe mtu wa kizazi cha leo ukija na staili kama hiyo ya Yohana mbatizaji ni lazima ukamatwe na ndugu zako na utapelekwa kwenye wadi za wagonjwa wa akili. Maana mahali ilipofikia dunia huwezi ukaipeleka kwa staili hiyo utakuwa pia hujaitende haki. 

Wakati nchi yetu ya Tanganyika inapata uhuru Elimu ya rais wa wakati huo JK Nyerere ya digrii mbili ilitosha kabisa kuendesha nchi na kwa sehemu kubwa mpaka leo hii bado watu wanamheshimu na kumuona kwamba alikuwa na akili nyingi sana. Lakini leo hii hao watu wenye digrii mbili ni watoto wadogo sana na wengine bado hawajapata kazi za uhakika. Kuna makanisa mengine yana vyama vya akina mama ambao wengi wao wamezidi miaka 45 na kutokana na mavazi yao kwa umri walionao wanataka na mabinti wa chini ya miaka 18 wavae mavazi kama wanayovaa wao,ambayo hata wao walipokuwa mabinti hawakuvaa mavazi kama hayo. Ni lazima tukubaliane kwamba kila nyakati zina watu wa aina yake na mitindo yake ya mavazi, hata siku hii ya leo unaweza ukavaa aina Fulani ya mavazi na watu wakakushangaa kwamba huyu ndugu mbona amevaa mavazi ya zamani sana. Hapo ni lazima tukubaliane kwamba lengo kubwa la mavazi ni kusitiri maungo ya miili yetu na suala la kujipamba au kupendeza ni kitu kingine. Mchungaji mmoja rafiki yangu alitoa onyo kwa akina mama wa kanisa lake kuacha kuwasumbua mabinti wanaokuja kanisani kuhusiana na mavazi na mapambo ya nywele aliwaambia ni afadhali kama wao wanaona shida kukaa nao basi waondoke wao na wasifanye kazi ya kuwafukuza vijana hao kwani hata wao wakati wanaingia kanisani hawakuwa kama walivyo sasa.

KANISA NI NINI?

Je kanisa ni jengo? Hapana! Kanisa ni mtu aliyezaliwa mara ya pili na ambaye amejazwa na roho mtakatifu na Mungu anamtumia katika kuujenga ufalme wake. Hii hasa ndio tafsiri halisi ya kanisa. Tukilijua hili litatuwezesha kufikiria namna ya kumtayarisha mkristo mmojammoja kibinafsi na hatimaye tukiwa kama kikundi ndio tunapoweza kuwa na kanisa imara la mahali. Hatutaweza kuacha jukumu la wito wetu kwa Mungu na kuanza kushindana na kupigana vijembe kwa mambo yasiyokuwa na maana baina ya watumishi au kufukuzana kwenye majengo ya dini zetu. Huu ni wakati wa kuwafundisha watoto wa Mungu jinsi ya kujipanga na kupambana na changamoto mbalimbali wakati dunia inakwenda na mabadiliko ya kasi kubwa. huu ni wakati wa viongozi wa kiroho kuzisoma nyakati na kujipanga kukabiliana na changamoto zinazolikabili kanisa kama mtu mmojammoja na kanisa kama kundi la watu wa mahali fulani  katika zama hizi za utandawazi na information Technolgy. Ni lazima tujue tunatumiaje maarifa yaliyoko duniani katika kuujenga ufalme wa Mungu na sio kupingana nao.



Wakati matumizi ya Internet yanaanza kuingia kuna baadhi ya makanisa walifanya maombi maalumu ya kufunga na kuomba kuzuwia mitandao ya yahoo na mingineyo isiingie katika nchi yetu kwa madai kwamba ni alama ya mpinga Kristo lakini walishindwa na leo hii wao wenyewe ndio wanaonufaika nayo kwa kuwasiliana na watumishi wenzao wan chi za mbali. Tukijua kwamba kanisa ni mtu basi ni lazima tuhakikishe tunamuandaa mtu kwa umakini mkubwa kulingana na mazingira yaliyopo, siku hizi kuwa mtu wa kiroho sio lazima uwe mtu wa kuzubaazubaa na kuvaa makoti makubwa kama mtu wa kutoka mashambani. Kuwa mtu wa kiroho siku hizi ni kuwa na maono na maono ni mipango ya namna utakavyoutumia wakati na mazingira yaliyopo katika kujenga ufalme wa Mungu, hapo haijalishi kwamba umeweka dawa nywele au una nywele zako za kipilipili. Hapa tutaangalia una uwezo gani wa kuwapelekea ndugu zetu wa mataifa ya kiarabu ambao bado hawajafikiwa na injili ukaongea nao

COPY AND PASTE SYNDROME (KUNAKIRI NA KUCHOMEKA)
Mojawapo ya mambo ambayo athali zake zinaonekana haraka sana katika utandawazi ni tabia ya kuiga haraka tabia na utamaduni wa mataifa mengine ambapo pengine huku kwetu ni tatizo.na vijana wengi wanafikiri kuwa kila kitu wanachofanya vijana wa ulaya kinakubalika na jamii ya watu wote walioko huko. ukweli ni kwamba yapo mambo mengi ambayo watu wa ulaya hawakubaliani nayo,lakini yakifika huku kwetu tunayaona ya maana na kuiga.

baadhi ya  mavazi ambayo hayakubaliki kabisa na inatakiwa kukabiliana nayo kwa nguvu za kiroho na kimwili.
Lakini pamoja na hayo yote hakuna sehemu hata moja ambayo inaweza kukwepa mabadiliko haya iwe kwa kutaka ama kwa kutokutaka. Kwa hali hiyo hata kanisa haliwezi kukwepa kuingia katika mabadiliko haya.woga wa aina yoyote utakuwa ni woga ambao hauna sababu,
Hii ni kwa sababu kanisa linavuna waumini wake kutoka katika jamii ya watu waliopo katika sehemu lilipo kanisa kwa hiyo ni lazima watu walio katika jamii hiyo wataingia kanisani wakiwa katika hali waliyonayo kabla mabadiliko ya kiroho yatakayoletwa kwa msaada wa roho mtakatifu na sio kwa nguvu ya kianadamu na roho mtakatifu atawafinyanga watu katika namna ambayo anaitaka mwenyewe kwa manufaa ya Mungu.
Ni jambo la kusikitisha sana kuona baadhi ya makanisa yanawazuwia watu wanaokuja makanisani kwao wakiwa katika hali Fulani ambayo inaoneana wameathiriwa na mambo ya utandawazi na tabia zake.

Kuongezeka kwa kasi ya uvukaji wa mipaka
baadhi ya miji na kisiwa cha Jamaika.


Katika eneo hili ni lazima litakuwa na faida lakini pia litakuwa na athari kwa kanisa na hasa makanisa ya mijini itakuwa ni vigumu sana kwa wachungaji kuwasimamia watu wanaowachunga kwa sababu hakutakuwa na utulivu wa watu makanisani kwani watu wengi watakuwa wanaingia na kutoka,na kila wanapotoka na kuingia watakuwa na mitazamo tofauti kulingana na mila na desturi za sehemu wanakotoka na sehemu wanazotembelea,kwa sababu ya changamoto hii ni lazima kanisa litegemee kukabiliana na migogoro mingi itakayohusiana na tabia mbaya za kuambukiza kutoka sehemu nyingine. hii ni changamoto kwa kanisa kuanza kujiandaa kukabiliana na mabadiliko bila kulalamika.



Maoni 2 :

  1. Kama huo ndiyo utandawazi hakika Dunia imeisha ni Bora Mungu afikirie upya aliapa hataangamiza tena Dunia lakini hivyo tunavyoenda kwa kweli ni Bora tu.

    JibuFuta
  2. Ni halali yao kwa kuwa dunia inatakiwa kupitia kipindi kama hiki kwa mujibu wa unabii. Unasemaje "Mungu afikirie upya"? Hawezi kusema ndiyo na hapana mara moja. Kwa muumini wa Kristo ni dalili ya kuja kwa Bwana wetu kulinyakua Kanisa. Tuko tayari tunamsubiri kwa hamu kubwa.

    JibuFuta