Jumamosi, 22 Aprili 2017

JINSI YA KUPOKEA UBATIZO WA ROHO MTAKATIFU



Tayari tumeshajifunza mambo mengi yamhusuyo Roho Mtakatifu, asili yake, huduma yake katika kanisa na faida ya kunena kwa lugha mpya inayoambatana na ubatizo huu wa Roho Mtakatifu.
Katika kulielezea hili, napenda kusema kuwa hakuna utaratibu maalumu uliowekwa katika Biblia kama kanuni ya kufuatwa katika kupokea ubatizo huu. Kwa sababu hiyo, hapa nitatoa mwongozo uwezao kusaidia kupokea na nitaongea kama vile neno la Bwana linavyosema.
KUSUDI LA KUTANGAZA UBATIZO LIWE LA KIBIBLIA.
“lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu. Nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na katika uyahudi wote na Samaria, na hata mwisho wa nchi” Matendo ya mitume 1:8
Ahadi ya Roho Mtakatifu ni kwa wote, ila wengi wameshindwa kupokea kwa kule kukusudia isivyopaswa juu ya kuhitaji kwao ubatizo huu.
Wengi wanamwomba Mungu kipawa hiki kwa kusudi la kusema kwa lugha tu, ili wafanane na watu wengine wanaonena kwa lugha.
Lugha mpya ni kitu muhimu mno kwa wanafunzi wa Yesu, lakini kusudi la ubatizo wa Roho Mtakatifu sio ili watu wanene kwa lugha mpya tu, ni zaidi ya hapo.
Mistari iliyotangulia hapo juu, inatuonyesha kusudi la kutaka kumpokea Roho Mtakatifu na utendaji wa nguvu zake. Ni lazima kila anayehitaji ubatizo huu, auhitaji tu ili awe shahidi mwaminifu wa Mungu. Na kwa sababu kuna nguvu inayojizalisha ndani ya Roho Mtakatifu lazima liwe lile la kumzalia Mungu matunda. Kupokea ubatizo huu na hatimaye kuendelea kukaa bila kufanya chochote kwa ajili ya kuong, yaani kuwafanya eza kuujenga ufalme wa Mungu huko ni kumzimisha na kumhuzunisha Roho wa Mungu. Kusudi kuu la kupata ubatizo huu ni kuwa shahidi mwaminifu wa kufa na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kufanya kile alichoagiza kabla ya kupaa kwake, yaani kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi na kuwafundisha kuyashika yote
LAZIMA UJUE KUWA NI HAKI YAKO KUPOKEA ROHO MTAKATIFU.
Biblia ni kitabu kilichojaa ahadi za Mungu kwa watu wake, kwa ujumla kuna ahadi zaidi ya elfu thelathini kutoka katika kitabu chwa mwanzo hadi kile cha Ufunuo. Kati ya ahadi hizo ni ile ahadi inayomhusu Roho Mtakatifu, iliyotolewa na Mungu kupitia kwa nabii Yoeli 2:28 “Hata itakuwa baada ya hayo, ya kwamba nitamimina  Roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume  kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono”.
hii ni ahadi kutoka kwa Mungu, kwenda kwa watu wake wa siku za mwisho, katika hili sote tunafahamu kuwa sisi ni watu wa siku za mwisho, kwani ahadi hii ilitimia duniani siku kumi tu baada ya Yesu kupaa. Katika matendo ya mitume tunasoma hotuba ya mtume Petro siku ya pentekoste, kati ya mambo aliyoyasema ni lile lililonenwa kwa kinywa cha nabii Yoeli, kuwa itakuwa siku za mwisho, asema Mungu, nitawamwagia watu wote Roho yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto. Basi kwa kuwa wewe na mimi tu waumini wa Mungu wa siku za mwisho, ni vema tuelewe kuwa ahadi hii ya kumpokea Roho Mtakatifu na nguvu zake inatuhusu, ni ahadi yetu. Waumini wengi wameshindwa kupokea ahadi hii, pale walipoisukumia ahadi hii mbali kwa watu wengine, nakutia moyo wewe na yeyote aliye mwanafunzi wa Yesu, kuomba kutimia kwa ahadi hii ndani yako kwa maana Roho Mtakatifu amekuja kwa ajili ya kila aaminiye.
LAZIMA KUWA NA KIU YA KUPOKEA ROHO MTAKATIFU
“Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, mtu akiona KIU na aje kwangu anywe” Yohana 7:37
Watu wengi wamekosa kupokea ahadi hii kwa kule kutojenga kiu ndani yao na kuhitaji kipawa hiki. Mtu yeyote anayehitaji kitu kutoka kwa Mungu ni lazima awe na kiu ya kupokea kile kitu kutoka kwa Mungu.
LAZIMA KUWA NA IMANI YA KUPOKEA.
Imani ni pale mtu anapokuwa na uhakika juu ya yale yatarajiwayo, ni kuwa na uhakika kuwa Mungu ana uwezo wa kufanya yale aliyoahidi.
Kwa imani tunasema kuwa tumepokea, tunayo na pasipo imani haiwezekani kabisa kumpendeza Mungu. Hatuwezi kupokea lolote kutoka kwake. Wasiwasi na mashaka ni adui mkubwa mno wa kupokea miujiza kutoka kwa Mungu. Kwa maana kila amwendeae Mungu akihitaji kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, ni lazima awe na imani ya kupokea yaani kuwa na uhakika kuwa Mungu aliye hai ana uwezo wa kufanya yale aliyoahidi.
ONDOA HOFU JUU YA KUPOKEA AHADI HII
Roho Mtakatifu amesemwa vibaya mno na watu wengi hasa pale ishara ya kunena kwa lugha inapojidhihirisha. Mara nyingine wenye hekima wa dunia hii, hudiriki kusema kuwa kunena kwa lugha ni mapepo! Kwa jinsi hii watu wengi, wameweza kuogopa hasa wanapoyasikia haya yakisemwa na viongozi wa madhehebu yao au vikundi vyao vya faragha. Kwa hofu hii, wengi hukubali kuhudumiwa ili wapokee ahadi hii ya Roho Mtakatifu huku wakiwa na hofu ya aina fulani hasa juu ya kunena kwa lugha mpya. Tukumbuke kuwa lile tuombalo kwa Mungu, ndilo tunalopokea, hivyo hakuna sababu ya kuwa na hofu wakati wa kupokea ubatizo huu.
Roho Mtakatifu ni nafsi hai ya Mungu nan i Mungu, hivyo anapoingia ndani huwa Baraka, hivyo badala ya watu kuwa na hofu ni vema watu kuchangamka na kuifungua mioyo yao ili kupokea kipawa hiki.
NI LAZIMA KUKIRUHUSU KINYWA CHAKO KINENE
“Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka” matendo 2:4
Hiki ni kipengele muhimu sana katika somo hili, wengi kwa kutokuelewa kile ninachoenda kikeleza sasa wameshindwa kupokea ubatizo wa Roho Mtakatifu pamoja na ishara ya lugha mpya. Waumini wengi wanaposikia juu ya lugha mpya wanafikiri kuwa ni lugha inayotamkwa na nguvu fulani ndani ya mtu. Kwa kufikiria hivi, hufikiri nguvu hiyo ndani ya mtu inaweza kumlazimisha kufunguka kwa kinywa cha mtu, na maneno yakaanza kutoka kama bubujiko la maji mwambani. Kwa fikira hizi potofu, wengi wametamani kupokea wasiweze kupokea. Mistali tuliyosoma inatuonyesha yale yaliyotokea wakati mitume wa Bwana, walipojazwa Roho Mtakatifu, walianza kusema kwa lugha mpya. Kwa maneno haya, tunaona kuwa mitume walifunua vinywa vyao na kuanza kusema na walipofanya hivyo, Roho Mtakatifu akawajalia maneno ya kusema. Maneno yanatoka kwa Roho Mtakatifu na kazi ya kuyasema ni ya mwanafunzi wa Yesu.
USIRUHUSU AIBU IKUTAWALE
Mambo mengi ya Mungu yanaenda kwa imani, na mambo ya imani ni upumbavu mbele za dunia. Ndio maana wapumbavu wa dunia hii hawaishi kusema kuwa hakuna Mungu. Tunapoongea juu ya ubatizo wa Roho Mtakatifu unaoambatana na kunena kwa lugha mpya. Dunia inatushangaa na kutucheka sana, mara nyingi mawazo ya dunia huingia ndani ya Kanisa la Mungu na kuwafanya waamini wengi kuanza kuyatazama mambo ya kiroho kama vile dunia inavyoyatazama, matokeo yake ni kanisa kupooza kwa kumzimisha Roho Mtakatifu.
Kwa kuwa lugha mpya ni moja ya mambo yasiyoeleweka katika dunia, basi watu wengi wanaona aibu kusema kwa lugha hiyo. Hivyo wanapojazwa Roho Mtakatifu na kuanza kunena kwa lugha mpya, huanza kuipeleka lugha hiyo katika akili zao na hapo kuiona lugha hiyo ni jambo lisilokubalika katika ustaarabu wao, na kuona kama kichekesho. Akili zao zinaposhindwa kukubaliana na hali hiyo, hujiona kuwa wanafanya jambo la kitoto, hivyo huamua haraka sana kunyamaza kimya. Hii ni kwa sababu ya kuona aibu. Jambo hili linapotokea huharibu tendo zima takatifu la kunena kwa lugha mpya. Maandiko yanasema kuwa atakayemwonea Yesu aibu, nay eye ataonewa aibu mbele ya Mungu na malaika zake.

Wengine wanashindwa kupokea kwa kule kusita kwao wakati wa mwanzo wa huduma hii. Hili hutokea mara tu mtu anapoanza kunena kwa lugha kwa mara ya kwanza. Wengi wanapousikia ule mtiririko wa ile lugha, hudhani kuwa wanaongea lugha yenye makosa, kwa hisia hii huruhusu ukavu ndani ya mioyo yao, na kushindwa kupokea. Ni vema unapoomba kitu kwa Mungu, inatakiwa kuwa kama mtoto mdogo na kumruhusu Mungu akufanyie kama anavyotaka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni