Jumatano, 1 Februari 2017

SOMO: ROHO MTAKATIFU NA MAMBO YAKE (1)


Mwl: Furaha Amon

Utangulizi:
Mwishoni mwa mwaka 1999 nilipata nafasi ya kwenda kuhubiri katika kanisa moja la Assemblies of God. 

Ni  umbali wa kama kilometa 78 kutoka katika mji ambao nilikuwa naishi kwa wakati huo. Kanisa hili lilikuwa na mtumishi Mchungaji ambaye tulikuwa tunafanya kazi wote serikalini lakini yeye baadae neema ilimzidi akaamua kuacha kazi na kuingia shambani kwa Bwana. 

Mtumishi huyu alikuwa ni kama baba yangu wa kiroho, kwa sababu ndiye niliokokea mikoni mwake na kiukweli ndiye aliyenilea kwa uangalizi wa karibu sana, tangu siku ile nilipokata shauri na kuamua kumfuata Bwana Yesu. Wakati huu Napata nafasi ya kwenda kuhubiri nilikuwa nakaribia miaka kumi kwenye maisha ya wokovu. Kwa kuwa ilikuwa ndio nasimama kwa mara kwanza kufanya huduma hiyo katika kanisa lake, ilibidi Mchungaji anitambulishe kwa washirika wake wapatao kama mia nne hivi kwa ibada ile ya asubuhi. 

Mchungaji aliwaeleza washirika wake jinsi alivyokutana na mimi na mwonekano wangu, aliwaambia kwamba mimi nilipohamishiwa kikazi sehemu aliyokuwepo tulikuja vijana kama sita, kati yetu mimi ndio nilikuwa naonekana mtata zaidi. Na kwa hiyo hawakuwa na mpango kabisa wa kunipa habari njema za wokovu. Na kwa kweli nakumbuka nilikuwa jeuri sana, na wasingeweza kunikabili wakati huo bila kukorofishana, na ilikuwa hatari sana kukorofishana na mimi wakati huo kwa sababu naweza kukuvizia na kukujeruhi japo kisirisiri. Na hii hali hata baada ya kuokoka ilikuwa bado ipoipo kidogo. Ilikuja kwisha baada ya kuoa, na kwa sababu mke wangu ni mtu mwenye huzuni nyingi sana, hapendi kabisa nifanye ukorofi wa aina yeyote ile, hivyo kila ninapotaka kufanya maamuzi fulani sijiangalii mwenyewe binafsi kama ilivyokuwa zamani, pamoja na kumuangalia Mungu lakini huwa namfikiria sana mke wangu asije akahuzunika. Lakini pamoja na familia yangu kwa ujumla.
Mchungaji mwenyeji wangu aliwaambia washirika wake kwamba, katika kundi letu walimlenga kijana mmoja wa kichaga ambaye alikuwa anaonekana anamwelekeo wa kuokoka mapema ingawa hakuweza kusimama katika wokovu baadae alianguka kiroho, na mwisho alifariki dunia bila kupata neema ya wokovu. 

Kwa sababu tulikuwa tunakaa chumba kimoja na huyo ndugu, nilikuwa naona juhudi zao za kumfuatilia mara kwa mara. Na mimi nakumbuka siku moja nilitafakari sana kuhusu uwepo wa Mungu. Nikajisemea moyoni kwamba, ngoja nifanye utafiti kujua kama kweli Mungu yupo au hayupo, ingawa nimelelewa katika familia ya kikristo lakini mwenyewe binafsi nilikuwa sina uhakika kama kweli Mungu yupo. Niliamini zaidi katika sayansi kwamba uhai ulijitokeza wenyewe kwa njia ya mageuzi.
 



Katika utafiti wangu  nikijua kwamba Mungu hayuko, nitachagua maisha ya kuishi kwa bahati nikakuta yupo. Kwa hiyo nikaona utafiti huu niufanye kwa makanisa yenye msimamo wa imani kali, na walokole wa kipentekoste nikaona ndio watakaonifaa. Kwa hiyo bila kuhubiriwa na mtu yeyote, nilimfuata huyo Mchungaji, na kumwambia mimi nataka kuokoka!. Mchungaji anawaambia washirika wake kwamba wao walishangaa na pia hawakuamini, wakajua shetani anataka kunitumia kuvuruga mpango wao kumpata mtu waliyemlenga. Kwa hiyo wakakubaliana kwamba nikikubali kuongozwa sala ya toba tu wataunganisha na ubatizo wa Roho Mtakatifu, bila hata kubatizwa kwa maji mengi, hata kama sijui habari za Roho Mtakatifu, mwenyewe anasema walitaka Roho Mtakatifu mwenyewe anibane kisawasawa. Na kweli siku iliyofuata walinipeleka katika kakanisa fulani kadogo kana washirika kama ishirini hivi. Wanaendesha  ibada zao katika shule moja ya msingi karibu ya sehemu yetu ya kazi. Na kweli baada ya kuongozwa sala ya toba alinipeleka sehemu moja yenye majengo ya ghorofa ambayo hajaisha ujenzi wake yametelekezwa bila kukamilika. Akanipandisha kwenye ghorofa ya pili, tukiwa watu wawili tu. Akaniambia piga magoti, akanielekeza maneno ya kusema, harafu akawa ananilazimisha niyaseme maneno hayo kwa kasi sana ya kujichanganya na nilipokuwa nikikosea ndio akawa ananiambia hiyo ndio lugha anayoitaka. Na kunihimiza endelea hivyohivyo kuongea vitu visivyoeleweka. Kwa kweli sababu nilikuwa katika utafiti sikufungua moyo wangu kabisa. Tulikaa eneo hilo la upweke karibu masaa matatu. Huku yeye anaendelea na maombi huku akinisikilizia mimi, nikiongea lugha ambavyo akili yangu haina matunda kabisa ni kama najifanyisha fanyisha tu. Kwa kweli maji ukiyavulia nguo huna budi kuyaoga. 

Ilibidi tu nifanye kujisemeshasemesha maneno yale huku magoti yakiniuma kama mtu aliyepewa adhabu ya kijeshi ya kutembelea magoti. Baadae aliniambia tayari nimepokea ujazo wa Roho Mtakatifu. Kwa kweli mpaka wakati huo mimi sikuwa nimeona badiliko lolote zaidi ya kujihisi kama mtahiniwa aliyefanya mtihani ambao hajafundishwa na hana uhakika wa majibu yake, nilikaa nikisubiri majibu ambayo sina uhakika nayo. Kila siku namshukuru sana Mungu kwa ajili ya ndugu zangu hawa. Japo wao walikuwa na vyeo vikubwa kazini, lakini walishuka chini na kunitumikia, kuhakikisha kwamba ninasimama. Nakumbuka ni kama walikuwa wanafanya zamu. Kuhakikisha sipati nafasi ya kushirikiana na marafiki zangu wa zamani. Kwa hiyo walihakikisha ninafuatana nao kwa kubadilisha kwenda kwenye huduma mbalimbali walikokuwa wanaitwa kuhudumu. Kwa kweli walikuwa na uwezo na nguvu kubwa sana kiroho, kiasi kwamba waliweza kuamuru mvua isimame ili wafanye kitu fulani na mvua ilitii. Hayo mambo yalikuwa yakifanyika mbele ya macho yangu. Wakikwambia nenda nyumbani kuna hiki na kile, ukienda unakuta kama vile walivyokwambia. Kwa ujumla hawa marafiki zangu walinifaa sana. Sasa pamoja na kunihakikishia kuwa nimepokea ujazo wa Roho Mtakatifu, ilichukua siku kama tatu hivi, nikiwa kwenye maombi yangu ya kubangaiza ghafla nikaona ulimi umekuwa mwepesi ninaongea lugha ambayo siielewi na nimeingiwa na hali fulani ya furaha na amani na kutamani kuendelea kuomba. Ndio nikaanza kujua kwamba huyo ndio Roho Mtakatifu ambaye Mungu alituahidi kwamba tutampokea. Kama ilivyokuwa kwangu mimi ndivyo ilivyo hata sasa. Watu wengi mno ndani ya makanisa wana kiu ya kupata ujazo wa Roho Mtakatifu, lakini bado kuna tatizo kubwa sana linalohusiana na kutomwelewa vizuri Roho Mtakatifu. Kwa kuwa kiu hii ni kubwa na tatizo la kutomwelewa Roho Mtakatifu ndani ya kanisa ni kubwa sana nimeona ni vema nitumie nafasi hii kutoa mchango kidogo wa kukusaidia kuelewa kwa kiasi habari za Roho Mtakatifu.
Kwa kupitia mafundisho haya, wale wenye kiu ya kumpokea Roho Mtakatifu na nguvu zake wataweza kupokea; na kwa wale wasio na kiu ya kupokea, kutokana na kutomwelewa Roho Mtakatifu na faida zake  wataweza kuumbiwa kiu na hatimaye kupokea. Ni matumaini yangu kuwa mafundisho haya, yatayaondoa kwa kiasi kikubwa matatizo yaliyopo ndani ya kanisa yanayohusiana na huduma hii ya Roho Mtakatifu.



Kwa leo naishia hapa, usikose kufuatilia somo hili katika sehemu inayofuata. Mungu akubariki sana, kwa maoni na ushauri tuwasiliane kwa namba 0677 609056





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni