Alhamisi, 27 Aprili 2017

WITO WA KARAMA ZA KUFANYA HUDUMA (2)


JE, KARAMA ZINGINE ZA HUDUMA ZILIKUWA KWA AJILI YA KANISA LA MWANZO TU?
Je, karama hizi za huduma zitatolewa kwa kanisa kwa muda gani? Yesu atazitoa kwa muda wote ambapo watakatifu Wake wanahitaji kuwezeshwa kufanya huduma. Hiyo ni mpaka atakaporudi. Kila mara kanisa linapokea Wakristo waliozaliwa upya wanaohitaji kukua, na sisi wengine tunahitaji kuendelea kukua na kukomaa kiroho daima.
Kwa bahati mbaya, kuna wengine ambao wamedhani kwamba kuna aina mbili tu ya huduma siku hizi – wachungaji na wainjilisti – kana kwamba Mungu amebadilisha mpango Wake. Hapana! Bado tunahitaji mitume, manabii na waalimu, kama kanisa la mwanzo lilivyohitaji. Sababu ya kutokuona mifano ya karama hizi katika kanisa kwa wingi duniani ni kwamba, Yesu ndiye anayetoa karama hizo kwa Kanisa Lake, si hili kanisa la siku hizi la bandia, lisilokuwa takatifu, lenye kuhubiri injili za uongo. Katika kanisa hili bandia utawapata wale wanaojitahidi – kwa unyonge sana – kujaza nafasi za baadhi ya karama za huduma (sana sana wachungaji na wainjilisti wachache tu), lakini hawafanani hata kidogo na zile karama za huduma ambazo zinatolewa na Mungu, ambazo Yesu hutoa kwa kanisa Lake. Tena, hawawawezeshi watakatifu kufanya matendo ya huduma, kwa sababu injili yenyewe wanayotangaza haileti utakatifu bali huwadanganya watu wafikiri tu kwamba wamesamehewa. Na hao watu hawana haja ya kuwezeshwa wafanye huduma. Hawana nia ya kujikana wenyewe na kuibeba misalaba yao.
UTAJUAJE KWAMBA UMEITWA?
Mtu anajuaje kwamba ameitwa kushika mojawapo ya nafasi hizo kanisani? Kwanza kabisa, atasikia mwito kutoka kwa Mungu. Atajikuta ana mzigo wa kutenda kazi fulani. Hii ni zaidi ya kuwa na haja ya kuona hitaji ambalo linaweza kutimizwa. Badala yake, ni njaa itokayo kwa Mungu, iliyoko ndani, yenye kumsukuma mtu kuingia katika huduma fulani. Kama kweli ameitwa na Mungu, hatatosheka mpaka aanze kutimiza wito wake. Wala haihusiani na watu kumchagua au kamati ya watu. Mungu ndiye anayeita.
Pili – Mtu aliyeitwa kweli atajikuta amewezeshwa na Mungu ili kutimiza kazi hiyo aliyopewa na Mungu. Kila nafasi katika zile tano ina upako wake wa KiMungu, wenye kumwezesha mhusika kufanya kile ambacho Mungu amemwita kufanya. Upako huja pamoja na mwito wenyewe. Kama hakuna upako, hakuna mwito. Mtu anaweza kutamani kufanya kazi katika huduma fulani, akaenda Shule ya Biblia kwa miaka minne kujifunza na kujiandaa kwa ajili ya huduma hiyo, lakini pasipo upako toka kwa Mungu, hana nafasi ya kufanikiwa.
Tatu – Ataona Mungu akifungua mlango au nafasi kwa ajili ya kufanyia kazi karama zake hizo. Kwa hali hiyo anaweza kujithibitisha kuwa mwaminifu, na hatimaye atapewa nafasi kubwa zaidi, majukumu makubwa zaidi na karama zaidi.
Kama mtu hajasikia mwito wa Mungu au msukumo wa ndani kuhusiana na mojawpao ya hizo karama tano za huduma, au kama hajisikii upako maalum wa aina yoyote ile ili kutekeleza kazi itolewayo na Mungu, au kama hakuna nafasi iliyojitokeza kutumia karama anayofikiri anayo, basi asijaribu kuwa kitu ambacho Mungu hajamwita kuwa. Badala yake, afanye bidii kuwa baraka katika kusanyiko lake, katika mahali anapokaa na kazini anakofanya. Hata ingawa hajaitwa kwenye “huduma tano” hizo, ameitwa kutumika kwa kufanyia kazi zile karama ambazo Mungu amempa, na anatakiwa ajithibitishe kuwa ni mwaminifu.

Ingawa Maandiko yanataja hizo karama tano za huduma, hii haimaanishi kwamba kila mtu anayeshika nafasi fulani atakuwa na huduma inayofanana na mwingine. Paulo aliandika kwamba kuna “tofauti za huduma” (1Wakor. 12:5), akionyesha uwezekano wa kutofautiana kati ya watumishi wanaoshikilia nafasi zinazofanana.Tena, inaonekana kuna viwango mbalimbali vya upako juu ya hao wanaoshikilia nafasi hizo. Basi, tunaweza kutofautisha kila nafasi kwa kiwango cha upako. Kwa mfano: Kuna waalimu ambao wanaonekana kuwa na upako zaidi kuliko wengine. Ndivyo ilivyo hata katika karama zingine za huduma. Mimi ninaamini kwamba mtumishi yeyote anaweza kufanya mambo yatakayosababisha ongezeko la upako juu ya huduma yake, kama kuwa mwaminifu na kujitolea sana kwa Mungu.

somo litaendelea

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni