Alhamisi, 27 Aprili 2017

WITO WA KARAMA ZA KUFANYA HUDUMA (6)

Nafasi Ya Mwalimu
Kulingana na orodha ya 1Wakorintho 12:28, nafasi ya mwalimu ni ya tatu. Mwalimu ni mtu ambaye ametiwa mafuta na Mungu kufundisha Neno la Mungu. Si kwamba kila mtu anayefundisha Biblia ni mwalimu kulingana na Agano Jipya. Wengi hufundisha kwa sababu wanajisikia kupenda kufanya hivyo, au wanajisikia kuwajibika kufanya hivyo, lakini mtu ambaye ana wito wa nafasi hiyo ya ualimu hupewa karama na Mungu kwa ajili ya kufundisha. Mara nyingi anapewa ufunuo wa Mungu kuhusu Neno la Mungu, naye anakuwa na uwezo wa kueleza Biblia kwa njia inayofanya ieleweke na kufanyiwa kazi.
Apolo ni mfano wa mtu aliyeshika nafasi hiyo katika Agano Jipya. Paulo alilinganisha huduma yake ya kitume na huduma ya Apolo ya kufundisha katika 1Wakorintho kwa kusema hivi:
Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. … Naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake (1Wakor. 3:6, 10b. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Mwalimu Apolo hakupanda wala kuweka msingi. Ila, yeye alitia maji mimea mipya kwa Neno la Mungu, na alijenga kuta kwenye msingi uliokuwepo.
Anatajwa tena katika Matendo 18:27, hivi:
Na [Apolo] alipotaka kuvuka bahari aende mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe, naye alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu. Kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.
Ona kwamba Apolo “akawasaidia sana” watu ambao walikuwa Wakristo tayari, na kwamba mafundisho yake yanaelezwa kuwa na nguvu. Mafundisho yenye upako kila wakati yana nguvu.
Huduma ya kufundisha ni ya muhimu sana kwa kanisa kuliko hata matendo ya miujiza au karama za kuponya. Hii ndiyo sababu imeorodheshwa kabla ya karama hizo katika 1Wakorintho 12:28.
Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa (Maneno mepesi kukazia).
Kwa bahati mbaya sana, waaminio wakati mwingine huvutiwa zaidi kuona uponyaji kuliko kusikiliza mafundisho dhahiri ya Neno ambalo litaleta kukua kiroho na utakatifu katika maisha yao.
Biblia inazungumza juu ya kuhubiri na kufundisha. Kufundisha ni kitu cha utaratibu na mpango, ila kuhubiri ni kitu cha uvuvio zaidi. Mara nyingi wainjilisti huhubiri. Waalimu na wachungaji mara nyingi hufundisha. Mitume huhubiri na kufundisha. Ni kitu cha kuhuzunisha kwamba waamini wengine hawatambui thamani ya mafundisho. Wengine hata hufikiri kwamba wakati pekee ambapo msemaji amepokea upako ni wakati wanahubiri kwa sauti kubwa na kwa mwendo wa haraka! Sivyo.
Yesu ni mfano bora kabisa wa mwalimu aliye na upako. Mafundisho Yake yalikuwa na sehemu kubwa sana katika huduma Yake kiasi cha watu wengi kumwita “Mwalimu” (Mathayo 8:19; Marko 5:35; Yohana 11:28).

Kwa maelezo zaidi kuhusu waalimu na kufundisha, ona Matendo 2:42; 5:21, 25, 28, 42; 11:22-26; 13:1; 15:35; 18:11; 20:18-20; 28:30, 31; Warumi 12:6, 7; 1Wakor. 4:17; Wagalatia 6:6; Wakolosai 1:28; 1Timo. 4:11-16; 5:17; 6:2; 2Timo. 1:11; 2:2 na Yakobo 3:1. Andiko la mwisho katika orodha hii linatuambia kwamba waalimu watapata hukumu kali zaidi, kwa hiyo wanapaswa kuwa makini sana kuhusu kitu wanachofundisha. Wanapaswa kufundisha Neno tu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni